×

Balama: Siyo Mara ya Kwanza Kumfunga Manula Bao la Mita 18

HAUWEZI kuwataja wachezaji waliocheza kwenye kiwango cha juu katika mchezo wa juzi wa watani wa jadi, Simba na Yanga bila ya kumtaja kiungo fundi, Mapinduzi Balama, aliyepewa jina la Kipenseli.

 

Kiungo huyo mwenye uwezo wa kukokota mipira kwenye goli la wapinzani, ndiye aliyefunga bao la kwanza ambalo liliwarudisha mchezoni Yanga wakati huo wanaongozwa kwa mabao 2-0 kabla ya Mohamed Banka kusawazisha na kufanya mchezo huo umalizike kwa sare ya mabao 2-2.

 

Balama alifunga bao hilo kiufundi kwa kufunga umbali wa mita 18 kwa shuti kali lililomshinda kipa wa Simba, Aishi Manula, ni mara baada ya kumtoka kiungo wa Simba, Mzamiru Yassin.

 

Mara baada ya mchezo huo kumalizika, Championi Jumatatu lilimtafuta Balama na kuzungumza naye, alisema: “Siyo mara yangu ya kwanza kumfunga Manula akiwa Simba, niliwahi kumfunga msimu uliopita nikiwa naichezea Alliance Schools, kwa aina hiyo ya bao.

 

“Hivyo siyo ajabu kwangu, kikubwa ninafurahi kuifungia timu yangu bao muhimu ambalo lilitusaidia kuturejesha mchezoni na kufanikiwa kusawazisha bao la pili kupitia kwa Banka.

 

“Bao hilo halikuwa la kubahatisha kwani nilimuona Manula amesogea mbele kabla ya kupiga shuti hilo ambalo yeye mwenyewe hakutarajia kama mimi ningepiga kwani alikuwa akiamini kuwa nitaendelea kukokota mpira.

 

“Lakini kutokana na kumjua vizuri Manula nilijaribu kupiga shuti hilo na zilikuwa juhudi zangu binafsi baada ya kuona timu imezidiwa nikajaribu kufanya uchoyo wa kujaribu kupiga.

 

“Nilikuwa nina uwezo wa kumpasia mchezaji mwenzangu kabla ya kupiga lakini nilijaribu kuwa mchoyo na mchezaji unatakiwa kuwa hivyo, pale unapoona una nafasi nzuri ya kufunga, basi unatakiwa kujaribu kama hivyo nilivyojaribu mimi,”anasema Balama.

 

Championi Jumatatu linakupa uchambuzi wa kiufundi wa kiungo huyo ambaye kwenye mchezo huo alionekana lulu kutokana na bao lake safi la umbali wa mita 18, ambazo ni hizi:

 

MTAALAMU WA PASI ZENYE MACHO

Balama alikuwa imara sana katika eneo la kiungo kwa dakika zote 90, alipiga jumla ya pasi 36 zilizofika kwa mtu, huku akitengeneza nafasi tatu za mabao kwa Ditram Nchimbi ambaye alishindwa kukaa eneo sahihi na kujikuta akishindwa kuhufikia mpira.

 

MZURI KWENYE KUKABA

Licha ya kuwa na kimo kidogo, lakini alikuwa hodari wa kupambana na kupora mipira, ambapo kwa dakika zote 90 alifanikiwa kupora mipira saba, akipora mipira minne kipindi cha kwanza na kipindi cha pili akipora mara tatu.

 

Mbali na hivyo, alifanikiwa kuzuia mashambulizi mara tatu ambapo kama siyo umahiri wake wa kufanya maamuzi ya haraka ingeweza kuleta hatari katika lango la timu pinzani lakini pia Balama alifanya takolini mara tatu.

 

HATARI AKIWA ANASHAMBULIA

Balama ni hatari sana akiwa analitazama lango la timu pinzani, ndiyo maana aliweza kufanya mikimbio mara 14 kuelekea katika eneo la Simba, ambapo moja kati ya hilo iliweza kuzaa bao, ambalo aliweza kufunga yeye mwenyewe.

 

Balama alifanikiwa kuingia mara nane katika boksi la Simba, ambapo mara zote alizofanya hivyo ilikuwa inaleta hatari katika lango la timu ya Simba, mbali na hivyo alfanikiwa kupiga mashuti mawili tu katika mchezo wote.

WILBERT MOLANDI NA ISSA LIPONDA

Leave a Comment