Ndege ya Iran Yadunguliwa na Jeshi la Marekani Karibu na Meli ya Kivita

Jeshi la Marekani limedungua ndege isiyo na rubani (drone) ya Iran baada ya kukaribia kwa umbali hatari meli ya kivita ya Marekani katika Bahari ya Arabia, tukio linaloashiria kuongezeka kwa mvutano wa kijeshi kati ya mataifa hayo mawili hasimu.
Kwa mujibu wa msemaji wa Jeshi Kuu la Marekani, Kapteni Tim Hawkins, ndege ya kivita aina ya F-35C iliyopaa kutoka kwenye meli ya kubeba ndege za kivita USS Abraham Lincoln, ililazimika kuidungua drone hiyo kwa kujilinda pamoja na kulinda usalama wa meli hiyo na wanajeshi waliokuwemo.
Hawkins alisema drone hiyo ilikaribia meli hiyo kwa umbali usio salama ikiwa na nia isiyoeleweka, huku meli hiyo ikiwa takriban maili 500 kutoka pwani ya Iran wakati tukio hilo lilipotokea.
Tukio hilo linatokea wakati Marekani ikiendelea kuimarisha uwepo wake wa kijeshi katika eneo la Mashariki ya Kati, hatua inayochukuliwa huku mvutano wa kisiasa na kiusalama kati ya Washington na Tehran ukiendelea kupanda.
Rais wa Marekani, Donald Trump, hivi karibuni ametishia kuchukua hatua za kijeshi dhidi ya Iran iwapo haitakubali kujadiliana kuhusu kuzuia mpango wake wa nyuklia. Hata hivyo, Ikulu ya White House imesisitiza kuwa diplomasia bado ni kipaumbele.
Akizungumza baada ya tukio hilo, Katibu wa Habari wa White House, Karoline Leavitt, aliliambia shirika la Fox News kuwa mazungumzo kati ya Marekani na Iran bado yanatarajiwa kufanyika baadaye wiki hii.
“Rais anaendelea kujitolea kufuata diplomasia kwanza, lakini ana chaguzi mbalimbali mezani, ikiwemo matumizi ya nguvu za kijeshi,” alisema.
Kwa upande wake, Kiongozi Mkuu wa Iran, Ayatollah Ali Khamenei, awali alionya kuwa shambulio lolote dhidi ya taifa lake linaweza kusababisha “vita vya kikanda”, kauli inayoonyesha hatari ya mzozo huo kusambaa zaidi katika eneo la Mashariki ya Kati.
Hadi sasa, Iran haijatoa tamko rasmi kuhusu kudunguliwa kwa drone hiyo.
Wachambuzi wa siasa za kimataifa wanasema tukio hilo linaweza kuongeza presha kwenye mazungumzo ya kidiplomasia yanayolenga kupunguza mivutano, huku dunia ikiangalia kwa karibu mustakabali wa uhusiano kati ya mataifa hayo mawili.

