MSANII wa Hip Hop, Emmanuel Elibariki Nay the True Boy, amekuja na kampeni mpya ya kuwasaidia watu wa hali ya chini ambayo inaitwa Nguvu ya Kitaa. Kampeni hiyo itaanza rasmi kesho siku ya kumbukumbu ya kifo cha Mwalimu Julius Nyerere, Oktoba 14, yenye dhamira ya kuwasaidia watu hao ambao wanasapoti kazi zake na za wasanii kwa ujumla.
Akizungumza na waandishi wa habari leo Oktoba 13, Nay amesema katika kampeni hiyo ambayo watatembelea Hospitali ya Tandale, nia ni kuwalipa fadhila watu wa kipato cha chini ambao wanafutilia kazi hizo lakini bado wanaishi katika mazingira magumu.
Aidha Nay amehitaji ushirikiano kutoka kwa wanahabari ili waweze kufanikisha jambo hilo kutokana na wasanii na vyombo vya habari kutegemeana na kutakuwa na matamsha ambayo watatembelea mikoa mbalimbali na wasanii ambao watatoa ushirikiano naye wakiwemo Young Killer Msodoki, Pam D, Chid Benz, Barnaba the Classic, Msaga Sumu, Chemical, Qboy, Gigy Money na Mkali Wenu. Pia ametoa rai kwa wasanii wenzake wengine ambao watataka kushirikiana naye kwamba mlango upo wazi.
“Muziki wa Bongo Fleva ulipofikia umefikishwa na walala hoi mtaani na ndiyo unatupa kiburi cha sisi kuishi tunavyoishi, “ alisema Nay.
Kampeni hiyo itakuwa na burudani mbalimbali kutoka kwa wasanii ambao wamejitolea kushirikiana na Nay wa Mitego ili kuendeleza mshikamano na watu ambao wanafuatilia kazi za wasanii hata kama kipato chao cha chini.
(PICHA: MUSA MATEJA/GPL)
Na Esther Msofe/GPL