Tarimba Aanika Kilichoibeba SportPesa TZ

ABBAS TARIMBA, Mkurugenzi wa Uendeshaji wa SportPesa Tanzania, amesema mafanikio makubwa ya kampuni hiyo yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na ushirikiano wanaoupata kutoka kwa wadau wake wa karibu ikiwa ni pamoja na Kampuni ya Global Publishers.

Ameyasema hayo leo alipotembelea Ofisi za Global Publishers zilizopo Sinza-Mori Dar es Salaam ambapo ziara hiyo imekuja katika kutimiza miaka mitatu kwa Kampuni ya SportPesa Tanzania.

“Tumekuwa tukifanya kazi kwa ukaribu na watu mbalimbali, na tulianza taratibu kwani kulikuwa kuna kampuni nyingine ambazo zinafanya kazi, ila kwa ushirikiano mkubwa ambao tumekuwa tukiupata kutoka kwa wadau na Kampuni ya Global hasa kwa upande wa magazeti ya michezo ambayo ni Championi na SpotiXtra, tumefanikiwa kwa kiasi kikubwa.

“Mbali na kufanya kazi kwa mafanikio makubwa pia tumekuwa tukilipa kodi kwa Serikali zaidi ya bilioni, hivyo sio kitu kidogo hasa ukizingatia kwamba maendeleo ya Serikali yanahitaji kodi nasi pia tumekuwa tukilipa kodi.

“Wadau ambao wapo pamoja nasi tunaomba ushirikiano wao kwani bado tunazidi kupambana ili kuwa bora na mambo yote tunayafanya kwa weledi na kuzingatia kanuni ambazo zipo,” amesema Tarimba.

Mbali na kusema hayo, Tarimba aliongeza kuwa amekuwa akiyafuatilia magazeti ya michezo yanayochapishwa na Global Group ambayo ni Championi na SpotiXtra, huku akiwasihi waandishi wazidishe juhudi zaidi.

“Nimekuwa nikiyafuatilia magazeti ya michezo ya Championi na SpotiXtra, mbali na kwamba ni washirika wetu ambao tunafanya nao kazi kwa ukaribu bado magazeti haya yamekuwa na muonekano bora, ubora wa kazi pamoja na yale yanayoandikwa hivyo, cha msingi ni kushikilia hapo ili kuzidi kuwa bora zaidi.”


PICHA NA MUSA MATEJA | Global Publishers

