
Wafanyakazi wa Benki ya Taifa ya Biashara (NBC) na wadau mbalimbali wa utalii mkoani Kilimanjaro wameanza safari ya kihistoria ya kupanda Mlima Kilimanjaro kwa lengo la kufikisha mashine ya kufanyia miamala (POS Machine) ya benki hiyo kwenye kilele cha mlima huo. Hatua hiyo mbali na kusogeza huduma za benki hiyo kwa wateja wake wanaotembelea mlima huo pia inalenga kudhihirisha umahiri wa teknolojia ya benki hiyo katika utoaji wa huduma zake kwa wateja.
Hafla ya kuiaga timu ya wafanyakazi hao wanaotarajiwa kushuka mlima huo Disemba 21, mwaka huu, imefanyika hii leo kwenye eneo la geti la lango la Marangu ikiongozwa na Mkurugenzi wa Idara ya Wateja wadogo na Binafsi  wa benki hiyo, Bw Elibariki Masuke sambamba na Mkuu wa Hifadhi ya Taifa ya Mlima Kilimanjaro (KINAPA), Kamishna msaidizi wa uhifadhi, Angela Nyaki.

Akizungumza wakati akibadhi mashine hiyo kwa timu ya wapanda mlima hao iliyoongozwa na Bw Dickson Busagaga ambae ni mdau wa habari mkoani Kilimanjaro, Bw Masuke alisema jitihada hizo ni muendelezo wa kampeni mpya ya “Tabasamu Tukupe Mashavu,” ya benki hiyo inayolenga kutoa fursa kwa wateja kufurahia pamoja na wapendwa wao wakiwemo ndugu, jamaa na marafiki katika Sikukuu za mwisho wa mwaka kupitia miamala iliyorahishwa kupitia benki hiyo.
“Tuko hapa kushuhudia historia mpya katika mapinduzi ya huduma za kibenki kupitia kampeni yetu “Tabasamu Tukupe Mashavu” tena kwa nguvu ambayo haijawahi kujaribiwa hapo awali yaani huduma ya kwanza kabisa ya mashine ya malipo (POS Machine)  juu ya Mlima Kilimanjaro.’’

“Safari hii ni zaidi ya kupanda mlima kwa dhana ya kimwili bali ni kielelezo cha kujitolea kwetu kwa uvumbuzi na matumizi ya kidijitali ambayo tunatoa kwa wateja wetu. Vituo sita kuelekea kwenye kilele cha Mlima huu mrefu kabisa barani Afrika na duniani kwa ujumla kwetu havimaanishi tu hatua za upandaji wa mlima huu bali pia ni vituo sita vya sifa ya kipekee vya mashine yetu ya POS ambavyo ni rahisi, haraka, salama, mahiri, teknolojia ya hali ya juu, na muhimu zaidi ni ishara ya maendeleo.’’
“Kila kituo kinatoa fursa kwa timu ya wafanyakazi wetu na wadau wetu wote wanaoshiriki zoezi hili kushiriki historia tajiri ya mlima wetu huu tunaojivunia kama hazina yetu ya kitaifa, na historia ya ukuu na urithi wetu.’’ Alibainisha.

Aliongeza kuwa wakiwa kwenye kilele cha mlima huo, timu hiyo  itafungua rasmi pazia la kuruhusu mashine hiyo ya POS kuanza kutoa huduma ya miamala kwa wateja kwa chaguzi mbalimbali za malipo ya kidijitali kama vile Apple Pay, Google Pay, Amazon Pay, Samsung Pay, na kadi yoyote ya benki.
Akizungumza kuhusu hatua ya benki hiyo , Kamishna Msaidizi Nyaki, pamoja na kuipongeza benki hiyo alisema ujio wa huduma hiyo kwenye mlima huo itarahisha upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wadau mbalimbali wanaotembelea mlima huo.
“NBC mnapeleka kifaa hiki sio tu kwenye kilele kirefu Afrika bali duniani. Niwapongeze sana kwa kuona umuhimu wa kutambulisha huduma hii duniani kupitia hifadhi hii mashuhuri. Mashine hii itasaidia wadau wa utalii kuweza kufanya miamala huko huko juu…tunashukuru sana kwa hatua hii,’’ alisema Kamishna Msaidizi Nyaki.
Aidha, Kamishna Msaidizi huyo pia aliwapongeza wadau wa habari mkoani humo kwa kuendelea kuhabarisha umma kuhusu upatikanaji wa mtandandao wa mawasiliano kwenye Mlima Kilimanjaro hatua ambayo imekuwa ikiwavutia wadau mbalimbali kutambulisha huduma zake kupitia huduma hiyo.

