The House of Favourite Newspapers

Yanga Yasalimu Amri Simba Bingwa

Wachezaji wa timu ya Yanga.

HATIMAYE benchi la ufundi la Klabu ya Yanga limeamua kukubali kuwa wapinzani wao Simba kwa msimu huu ndiyo mabingwa huku wao sasa wakijipanga kuelekeza nguvu zao katika michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika.

 

Yanga ndiyo mabingwa watetezi wa ligi kuu baada ya kuutwaa msimu uliopita wakiwazidi Simba kwa mabao ya kufunga lakini kwa msimu huu hadi sasa wanakamata nafasi ya tatu kwenye msimamo wakiwa na pointi 48 ambazo ni pointi 17 nyuma ya Simba wanaongoza ligi wakiwa na pointi 65.

 

Akizungumza na Championi Jumatano, muda mfupi baada ya kurejea kutoka nchini Algeruia, Kocha Mkuu wa Yanga, Mkongomani Zahera Mwinyi alisema kwa sasa wamekubali kuwa wapinzani wao ndiyo mabingwa wa ligi huku wao wakielekeza nguvu sasa katika michuano ya kimataifa ambayo wanashiriki.

 

“Kwa hali ilivyo kwa sasa Simba ndiyo mabingwa wa ligi kwa msimu huu huku sisi tumepanga kwa sasa kuelekea nguvu zetu katika michuano ya kimataifa ambapo tunashiriki Kombe la Shirikisho Afrika.

“Tunaelekeza nguvu huko kwa sababu hapa Tanzania hatuwezi kuwa mabingwa lakini pia Kombe la FA tumeshatolewa,” alisema Zahera.

Akizungumzia juu ya mwanzo mbaya wa kikosi hicho katika mchezo wake wa hatua ya makundi Kombe la Shirikisho Afrika, Mkongomani huyo alisema:

 

“Tulienda na wachezaji ambao hawana uzofu na michuano hii na ndiyo sababu iliyochangia kwetu kufungwa mabao 4-0 mbele ya wapinzani wetu, licha ya kwamba walifuata maelekezo ya kile ambacho niliwaambia.

 

“Wachezaji wale muhimu tuliwaacha hapa Dar, utaona jinsi jambo hilo lilivyoweza kuchangia sisi kupoteza mechi yetu ya huko. Nimepanga kuongea na uongozi ikiwezekana kwamba kuwe na timu mbili ambapo moja itaenda Mbeya kucheza na Mbeya City (kesho Alhamisi) halafu ikimaliza iende pia Morogoro kucheza na Mtibwa.

 

“Wakati huohuo pia kuwe na timu ambayo nitabaki nayo hapa Dar ambayo itajumuisha wale wachezaji ambao hawakwenda Algeria ambao nitakaa nao na kuzungumza, hii timu nitawapa mafunzo kuhakikisha kwamba inafanya vyema kwenye mchezo wetu dhidi ya Rayon Sport.

 

“Nafanya hivyo kwa sababu nataka nguvu zetu nyingi tuelekeze huko kwenye michuano ya kimataifa kwani ndiyo nafasi pekee ambayo imebaki kwetu kuona tunashiriki michuano ya Afrika kwa msimu ujao, kwani hakuna sehemu nyingine zaidi ya huku hivyo yatupasa kuweka nguvu zaidi,” alisema Mkongomani huyo.

Waandishi: Omary Mdose, Ibrahim Mressy na Sweetbert Lukonge

Comments are closed.