The House of Favourite Newspapers

Kigogo Yanga Awashangaa Waliojiuzulu

Makamu Mwenyekiti wa Yanga SC, Clement Sanga (katikati).

KAIMU Mwenyekiti wa Klabu ya Yanga, Clement Sanga, ameonyesha kushangazwa na hatua zilizochukuliwa za kujiuzulu kwa wajumbe wawili wa kamati ya utendaji ya klabu hiyo.

Hivi karibuni, wajumbe hao wawili ambao ni Salum Mkemi na Hashim Abdallah, walitangaza kujiuzulu kutokana na sababu mbalimbali yakiwemo matokeo mabaya ya timu hiyo.

Sanga amesema: “Tupo kwenye vita hatutakiwi kukimbia mapambano, tunatakiwa kupambana hadi mwisho halafu tuwaambie waliotuchagua tumefikia hapa, wao ndiyo watakuwa na maamuzi tufanye nini baada ya kufika hapo na baada ya hapo kitatokea hicho kinachotakiwa kutokea kwa maslahi mapana ya Yanga.

“Ukiangalia sababu ambazo zimetolewa ambazo zimekuwa wazi na naweza kuzizungumzia, kuna mjumbe amejiuzulu na amesema ameona kwamba tumeishia nafasi ya tatu kwenye ligi kwa hiyo anawajibika.
“Nimeangalia nimeona kila mwaka hata klabu nyingine zingekuwa zinafanya mabadiliko ya uongozi, kwa sababu hazijamaliza katika nafasi ambazo walijiwekea malengo.

“Waliowachagua wanajua kwa nini wamesema vile lakini wao ndiyo watakuwa na hoja nyingi za kuhoji kwa nini viongozi wao wamejiuzulu.”

Comments are closed.