Jaji Mkuu wa Tanzania, Mhe. Profesa Ibrahim Hamis Juma amekitaka Chama cha Wanasheria Wanawake Tanzania (TAWLA) kufanya tafiti katika baadhi ya Sheria ambazo zinahitaji marekebisho ili kuweza kuongeza uzito wa mabadiliko hayo.
Mhe. Jaji Mkuu aliyasema hayo mapema Agosti 17, alipotembelewa na wajumbe wapya wa Baraza la Uongozi wa TAWLA, ambao waliongozwa na Mwenyekiti wao, Bi. Athanasia Soka na Mkurugenzi wa TAWLA, Bi. Tike Mwambipile, waliofika kwa ajili ya kujitambulisha rasmi.
Akizungumzia kuhusu mabadiliko hayo ya Sheria, Jaji Mkuu alisema yanawezekana kufanyika endapo utatifi wa kina utafanyika ili kuongeza uzito wa mabadiliko hayo, “ni vizuri unapotaka kufanya mabadiliko kisheria kufanya utafiti ,tunaweza kufanya kwa kushirikiana,” alisema Jaji Mkuu.
Awali akizungumzia kuhusu mabadiliko ya Sheria yanayohitajika, Mkurugenzi huyo wa TAWLA, Bi. Tike Mwambipile, aliitaja Sheria ya ndoa.
“Katika sheria hii mathalani kumekuwa na mgawanyo wa mali usio sawa hususani pale ambapo mwanaume inapothibitishwa ndiye anamiliki mali hupata asilimia nyingi na mwanamke hupata asilimia chache wakati ikithibitika mwanamke ndiye anamiliki mali hugawanywa asilimia 50 kwa asilimia 50,” alisema Bi. Mwambipile.
Mbali na sheria ya ndoa, Wajumbe hao pia waliitaja sheria ya Mtoto kuwa miongoni mwa Sheria zinazohitaji kufanyiwa marekebisho hususani kumlinda mtoto pale anapofanyiwa Ukatili wa kijinsia mfano kubakwa.
Aidha; Mhe. Jaji Mkuu aliwataka pia kuweka rekodi za takwimu vizuri na kuongeza kwamba hilo ni eneo ambalo, Mahakama inahitaji kufanya kazi kwa ushirikiano na chama hicho.
Katika mazungumzo hayo viongozi hao, walizungumzia jinsi ya kuweza kushirikiana katika kesi za ubakaji, namna ya kumaliza kesi za migogoro ya mirathi kwa kutumia upatanishi na usuluhishi kabla ya shauri kufunguliwa Mahakamani na uendeshaji wa kesi za ukatili wa kijinsia (GBV).
Na Magreth Kinabo, Mahakama.
Comments are closed.