The House of Favourite Newspapers

NKANA WACHEZA PATA POTEA DAR

NKANA walitua Jijini Dar es Salaam usiku wa kuamkia jana huku Kocha wao, Beston Chambeshi akitamba kucheza pata potea kwa kushambulia mwanzo mwisho dhidi ya Simba Jumapili.

 

Mabingwa hao wa Zambia wanaongoza mabao 2-1 baada ya kushinda mchezo wa awali wa raundi ya kwanza kwao na sasa wanahitaji sare au suluhu kusonga mbele hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

Simba inahitaji ushindi wa bao 1-0 ili kusonga mbele kwenye hatua ya makundi ya michuano hiyo mikubwa Afrika ingawa wenyewe wamesisitiza kwamba ni kufa na kupona.

 

“Kuruhusu bao ni jambo la kawaida kwenye haya mashindano makubwa, cha muhimu sasa ni mchezo wa Jumapili na ndio maana tumewahi kuzoea hali ya hewa.

 

“Itakuwa ni mechi nzuri sana ya kushambulia, hawatajilinda kama walivyofanya kwenye mechi ya kwanza.

 

“Watafunguka na kushambulia na sisi tutatumia faida hiyohiyo,” alisema Chambeshi na kuongeza kwamba kiungo Harrison Chisala ni miongoni mwa mastaa atakaowatumia kumaliza mchezo huo.

 

Alisema mchezaji huyo ni chipukizi lakini amekuwa staa kwenye mechi za awali za kimataifa walizocheza na yuko kwenye mipango yake ya kikosi cha kwanza cha kuipindua Simba.

Comments are closed.