The House of Favourite Newspapers

BATA LA DIAMOND, TANASHA NYEGEZI LAACHA HISTORIA

Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz na Mpenzi wake, Tanasha Donna Barbieri ‘Zahara Zaire’

MWANZA: MKALI wao Bongo Flevani, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ bado ameendelea kutengeneza vichwa vya habari, safari hii amekuwa gumzo kwa kujiachia vilivyo na mpenzi wake, Tanasha Donna Barbieri ‘Zahara Zaire’ maeneo ya Nyegezi, Mwanza na kuacha historia.  Kikubwa zaidi kilichozua gumzo kwa Diamond ni baada ya kuonekana akiwa kwenye pikipiki kubwa za kukodi huku akiwa amempakiza mrembo huyo wikiendi iliyopita alipokuwa amekwenda kwenye Tamasha la Wasafi.

“Ni maisha f’lani hivi ambayo tumezoea kuyaona wakiyafanya wenzetu nje ya nchi kwenye video zao lakini kwa huku Nyegezi Mond kaandika historia,” alisema Juma Bwiru. Mkali huyo alionekana akiwa anaendesha pikipiki hiyo huku akiwa amempakiza Tanasha ambaye mkono mmoja alikuwa ameshika chupa kubwa ya kilevi, mwingine akiwa amemshikilia Diamond tumboni kimahaba.

Mbali na eneo hilo, Diamond amekuwa gumzo katika viunga mbalimbali vya Jiji la Mwanza ambavyo ametembelea akiwa na Tanasha huku watu wengi wakionekana kutaka kumuona kwa karibu mrembo huyo ambaye amechukua nafasi kwa Diamond aliyemwagana na wazazi wenzake, Hamisa Mobeto na Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’.

Hata hivyo, kutokana na ulinzi mkali wa msanii huyo, imekuwa ni vigumu sana kwa mashabiki kuweza kumsogelea mrembo huyo kutoka Kenya. Mbali na maeneo tofauti ya Jiji la Mwanza ambayo Diamond alijiachia, funga kazi zaidi ilikuwa ni kwenye Hoteli ya Gold Crest aliyofikia ambapo aliponda raha kwa kula na kunywa vinywaji vya gharama pamoja na kruu nzima ya Wasafi Classic Baby (WCB).

Stori:Mwandishi Wetu, RISASI MCHANGANYIKO

Comments are closed.