Benki ya Biashara ya DCB imetoa shukurani kwa waheshimiwa wabunge pamoja na
mheshimiwa spika kwa kufanikisha zoezi la uuzwaji wa hisa zao lililofanyika hivi karibuni kwa
mafanikio.
Akizungumza wakati wa mahojiano maalumu jijini Dodoma sambamba na ziara ya uongozi
wa juu wa DCB ulioongozwa na Mwenyekiti wao wa Bodi bungeni juzi, Mkurugenzi Mtendaji wa
DCB, Godfrey Ndalahwa alisema wabunge kama wawakilishi wa wananchi wamesaidia sana
kwa taarifa za uuzaji wa hisa zao kuwafikia wananchi wengi.
Alisema mafanikio ya uuzaji wa hisa yaliyoifanya benki kuongeza mtaji wake yatasaidia mpango
mkakati wao wa kutanua wigo wa huduma zao wakitarajia ndani ya miaka mitano kuwafikia
watanzania wengi huku wakiwekeza zaidi katika huduma za kidigitali.
“DCB ilianza mpango wake wa kujitanua kutoka jijini Dar es Salaam miaka miwili iliyopita, safari
ya kujitanua inaendelea, tumeshafika Dodoma na maeneo ya karibu, mfumo wetu unaotusaidia
ni kutoa huduma bora kwa bei nafuu tukiwekeza zaidi katika mfumo wa kidigatali hivyo kuwa na
matawi machache na kuweka vituo vingi vya huduma sehemu mbalimbali nchini,” alisema.
Zoezi la uuzwaji wa hisa za DCB lilizinduliwa Novemba 12,2018 na kuhitimishwa Januari 31,
2019 ambapo hisa 36,635,435 ziliuzwa ikivuka kiwango cha hisa 33,913,948 zilizopangwa awali.
Comments are closed.