Bosi Simba SC: Tutawang’oa Waarabu Kwao
BAADA ya sare ya mabao 2-2, uongozi wa Simba umesema kuwa umeanza maandalizi ya mchezo wa marudiano dhidi ya Al Masry ya Misri huku akitamka kuwa wanakwenda kubadili matokeo ugenini.
Kauli hiyo ya kishujaa aliitoa Kaimu Rais wa Simba, Salim Abdallah ‘Try Again’ mara baada ya kumalizika kwa mechi hiyo ya Kombe la Shirikisho Afrika kwenye Uwanja wa Taifa.
Abdallah amesema anawapongeza wachezaji wake kupambana dakika 90 na kupata matokeo hayo lakini wakienda ugenini na kujitoa kwa moyo mmoja, basi watabadili matokeo.
“Bado tuna nafasi kubwa ya kwenda Misri na kubadili matokeo kwa maana ya kuwaondoa Al Masry na hilo litawezekana kama wachezaji wataonyesha kiwango kikubwa kama hiki walichokionyesha.
“Kiukweli vijana wetu walipambana sana katika mechi hiyo, ninaamini kama siyo mvua kuharibu uwanja, basi tungewafunga wapinzani wetu kutokana na presha kubwa ya wachezaji waliyoipeleka golini kwa Waarabu,” alisema Abdallah.
Comments are closed.