HABARI njema kwa mashabiki wa Yanga ni kuwa mshambuiliaji wao, Mzambia, Obrey Chirwa, amerejea kikosini na kuanza mazoezi ya pamoja na timu hiyo kwa ajili ya kujiandaa na mechi ya pili ya hatua ya makundi Kombe la Shirikisho Afrika.
Yanga inatarajiwa kujitupa kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam keshokutwa Jumatano saa moja usiku kwa ajili ya pambano hilo dhidi ya Rayon Sports ya Rwanda.
Timu hiyo itaingia uwanjani ikiwa na hasira ya kupoteza mchezo wa kwanza wa michuano hiyo baada ya kufungwa mabao 4-0 na USM Alger ya Algeria.
Akizungumza na Championi Jumatatu, kocha mkuu wa timu hiyo, Mkongoman, Zahera Mwinyi, alisema Chirwa ameripoti mazoezini na kufanya na wenzake kwa siku mbili mfululizo Ijumaa na Jumamosi kwa ajili ya mchezo huo.
Zahera alisema, kurejea kikosini kwa mshambuliaji huyo kumeongeza hamasa kubwa katika timu yake hiyo katika kuelekea kwenye mchezo huo ambao wanahitaji ushindi wa nyumbani.
Mkongoman huyo aliwataja wachezaji wawili ambao tangu wameanza maandalizi ya mechi hiyo na Rayon hawajaripoti mazoezini ni Ibrahim Ajibu na Hajji Mwinyi wanaodaiwa kugoma kwa kudai mishahara yao mitatu.
“Nafurahi kuona baadhi ya wachezaji wakibadili maamuzi ya kugomea mazoezi akiwemo Yondani na Chirwa ambao wenyewe katika mazoezi ya awali hawakuwepo lakini hivi karibuni waliripoti na kuanza na wenzao.
“Nasikitika kuona wachezaji kama Ajibu na Mwinyi wenyewe tangu tumeanza mazoezi hawakuripoti, lakini mimi kama kocha ninaendelea kufanya mazoezi na hawa wachezaji nilionao nikiwasubiria waliopo Morogoro,” alisema Zahera.
Wilbert Molandi, Dar es Salaam
Comments are closed.