The House of Favourite Newspapers

DARAJA LAANGUKA, LAUA WAFANYAKAZI TISA COLOMBIA

DARAJA liliokuwa linajengwa nchini Colombia limeanguka na kuua wafanyakazi tisa na kuwajeruhi wengine watano. Daraja hilo lililoko eneo la Chirajara lilikuwa liwe sehemu ya barabara kuu inayounganisha mji mkuu wa Bogota na jiji la Villavicencio.

Picha za tukio hilo zinaonyesha eneo kubwa la daraja hilo lenye urefu wa mita 450 likiwa limeanguka. Waziri wa Usafirishaji Germán Cardona alisema chanzo cha ajali hiyo kinachunguzwa. Mfanyakazi mmoja miongoni mwa waliojeruhiwa alisimulia tukio hilo na kusema:

 

 

“Kila mtu alianza kupiga kelele kuwa daraja linaanguka, sikuwa na muda wa kufanya chochote na kisha nikasikia kitu kinanipiga kichwani,”

 

Luis Alvarado aliliambia gazeti la El Tiempo. Maofisa wa ujenzi walisema kwamba bahati nzuri si wafanyakazi wengi waliokuwa juu ya daraja hilo wakati linaanguka kwani walikuwa wanapata maelezo kuhusu usalama eneo hilo.

 

Daraja hilo ni sehemu ya mpango mkubwa wa kuendeleza njia inayoelekea Bogota katika mbuga za mashariki ili kuifanya iwe na njia mbili. Kazi iliyopangwa inajumuisha ujenzi wa njia 18 za ndani ya milima, madaraja 42 pamoja na kamera za kurekodi matukio.

 

 

Njia iliyopo ambayo ni nyembamba hufungwa kila mara kutokana na malori yanayopeleka mizigo Bogota yanapoharibika na kukwamisha magari mengine kupita.

Comments are closed.