The House of Favourite Newspapers

DIAMOND AMLIZA MAMA MOBETO!

Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’

USHUHUDA alioutoa hivi karibuni mkali wa Bongo Fleva, Nasibu Abdul ‘Diamond Platnumz’ kuhusu maisha yake, umekuwa mwiba mkali kwa mama wa mwanamitindo Hamisa Mobeto, Shufaa Lutiginga kutokana na kuonesha dharau kwa binti yake.  Diamond alizua gumzo la aina yake mwishoni mwa wiki iliyopita baada ya ‘klip’ iliyomuonesha akizungumzia kile alichokiita ‘mwaka wake mbaya’ kuonekana kumshusha thamani mzazi mwenzake, Mobeto kwa kumuita mchepuko (side chick) pamoja na mwanaye (side kid).

Baada ya kuzungumza maneno hayo, mitandaoni ‘kulichafuka’ ambapo wasiompenda Mobeto walianza kumshambulia mrembo huyo kwa kuitwa mchepuko pamoja na mwanaye. Baada ya maneno kuwa mengi mitandaoni huku kila mmoja akizungumza lake, mwanahabari wetu alimvutia waya mama Mobeto ili kumsikia anazungumziaje kauli hiyo ya ‘mkwewe’ iliyoonesha dharau kwa bintiye pamoja na mjukuu wake ambapo alipopokea simu alionesha kutofurahishwa.

“Jamani inauma na kwa kweli nisingependa hayo mambo jamani kuyaongelea mimi… jamani naombeni sana mtafuteni huyo mwenyewe aliyesema au Mobeto tafadhali, niacheni mimi nipumzike,” aliongea kwa sauti iliyochanganyikana na kilio moyoni kuonesha ana machungu na kutofurahishwa na jambo hilo.

Ijumaa Wikienda lilijaribu pia kumtafuta Mobeto ili kumsikia anazungumziaje ishu hiyo, lakini bahati mbaya simu yake iliita bila kupokelewa.

TUJIKUMBUSHE

Kwenye klip hiyo ya Diamond inayodaiwa kuwa ni mahojiano yake aliyoyafanyia nje ya nchi, Diamond alisikika akijilaumu kuwa mwaka 2017 ulikuwa mbaya maishani kutokana na matukio mabaya yaliyomtokea. Alisema, mwaka huo ndiyo ambao aligombana na mpenzi wake wa muda mrefu, Zarinah Hassan ‘Zari The Boss Lady’ aliyezaa naye watoto wawili, mmoja wa kike.

Alisema hayo yote yalitokea baada ya kuchepuka na Mobeto na kujikuta amempa ujauzito na hata Zari alipojaribu kuhoji baada ya kusikiasikia fununu, alijaribu kumficha ili kulinda uhusiano wake, lakini hata hivyo jipu lilikuja kupasuka baada ya Mobeto kuvujisha picha zao wakiwa kimahaba chumbani, jambo ambalo lilimharibia sana.

Mwishoni kwenye klip hiyo, Diamond alisikika akiwaasa vijana wote wenye wapenzi wao ‘serious’ au wenye wake zao, kuwa makini pindi wanapokuwa na michepuko ili kuepuka kupata watoto wa mchepuko kama ilivyomtokea yeye, jambo ambalo limekuwa baya maishani.

Comments are closed.