The House of Favourite Newspapers

 Fela: Wadau njaa walinigombanisha na nature!

HUWEZI kuizung-umzia historia ya muziki wa Bongo Fleva bila kutambua mchango wa Said Fela. Ni mdau wa muziki huu tangu kitambo. Amefanya mengi, makubwa na anaendelea kufanya hadi sasa licha ya kuwa na kofia nyingine ya siasa; Diwani wa Kata ya Kilungule, Temeke jijini Dar.  Fela amewahi kuwasimamia wasanii wengi kama TMK Wanaume Family, Yamoto Band na mpaka sasa akiwa anawasimamia Chege na Temba kupitia Kundi la TMK Wanaume.

Fela amezungumza mengi na Ijumaa ShowBiz, yanayohusu muziki ambapo pamoja na mambo mengine, amefunguka kuwa, hakuwahi kugombana na msanii wake yeyote bali ‘wadau njaa’ ndiyo walikuwa wakiwagombanisha kwa kupeleka manenomaneno kwa wasanii wake.

Akiwa na TMK Wanaume Family, baadhi ya wasanii wakiongozwa na Juma Nature walijiengua na kuanzisha kundi lao, lakini kama hiyo haitoshi, wasanii wake wa Yamoto Band akiwemo Aslay, Beka One, Enock Bella na Maromboso, wote walisambaratika na kusababisha kundi hilo kuvunjika.

Fela anasema, kitendo cha baadhi ya wadau wa muziki nchini kuingilia maisha kati ya msanii na uongozi wake, kimesa-babisha mdau huyo kuto-kuwa na mae-lewano mazuri na baadhi ya wa-sanii husika na bahati mbaya hata wa-kiwa-fitini-sha, wa-sanii hao wame-kuwa wakikosa msaada baadaye.

Kwa sasa Fela ni kiongozi wa Kundi la TMK Wanaume, kundi ambalo lilianzishwa baada ya baadhi ya wasanii kujiengua katika Kundi la TMK Wanaume Family na kuanzisha TMK Wanaume Halisi.

Akizungumza na Ijumaa ShowBiz, Mkubwa Fela anasema katika kipindi chote ambacho amekuwa akiwasimamia wasanii kisha baadhi kuondoka, yameibuka meneno mengi ikiwemo ya kuwanyonya wasanii kwa kutowapa stahiki zao jambo ambalo halina ukweli wowote.

Ungana na Ijumaa ShowBiz katika maswali na majibu hapa chini;

Ijumaa: Mkubwa Fela najua mbali na kuwa meneja wa TMK Wanaume, ni meneja pia wa Wasafi Classic Baby (WCB) na wikiendi hii mna shoo ya Wasafi Festival 2019, hebu tuambie kwanza mmejipangaje?

Fela: Kikubwa watu wanachotakiwa kujua ni kwamba hakuna tamasha lililowahi kutokea ambalo limekusanya wasanii 34 ambao watapiga shoo siku moja hivyo basi utofauti wetu tukaona turekebishe muda wa kuanza kwa hili tamasha, litaanza saa 1:00 kamili asubuhi hivyo basi watu wawahi tu ili wajionee utofauti wa tamasha hili na matamasha mengine ambayo yaliwahi kufanyika hapa Bongo.

Ijumaa: Na katika listi hiyo ya wasanii 34 kuna wasanii wa zamani pia, ni nini mmekiona hasa kinaweza kuwa na ushawishi kutoka kwa wasanii hao?

Fela: Kwanza kikubwa zaidi kilichofanya tuwaweke wasanii hawa wa zamani, tunahitaji kuwarudishia matumaini na watambue kwamba muziki wao bado unaishi masikioni mwa watu na wana mashabiki wengi sana mitaani mwetu.

Ijumaa: Na kuna tetesi zilikuwepo hapo kipindi cha nyuma kuwa wewe na Juma Nature hamko na maelewano mazuri, ni nini kimetokea mpaka na yeye ametajwa kwenye listi hiyo ya watakaopafomu hapo kesho?

Fela: Kwanza kabisa mimi binafsi sijawahi kugombana na msanii wangu yeyote bali wadau njaa ndiyo ambao walinigombanisha na baadhi ya wasanii wangu ambao mliona nina tofauti nao, kwanza mimi nigombane nao kwa sababu zipi wakati mimi napata ugali wangu na huku nikihitaji pia na wao wapate ugali wao wa kila siku na maisha yao yasonge mbele, lakini wasanii hao kuna watu wakaja kuwashika masikio na kuanza kuwapandikiza maneno ambayo siyo mazuri kwa kweli na ndiyo chanzo cha mambo yote kikawa ni hicho. Narudia tena mwandishi; wadau njaa ndiyo ambao walinigombanisha na wasanii wangu.

Ijumaa: Basi mkubwa tumalizie na je, unaweza kuendelea kufanya kazi na Nature au ndiyo itaishia kwenye hii Wasafi Festival?

Fela: Kama nilivyosema kwamba sijawahi kugombana na wasanii wangu kwa hiyo kazi zitaendelea kama kawaida, kikubwa cha kuwasisitiza watu ni kuwahi tu hiyo Jumamosi (kesho) kwani kuna mambo mengi sana yatakayofanyika siku hiyo.

STORI: AMMAR MASIMBA

Comments are closed.