The House of Favourite Newspapers

Kasi Ya Yanga Ubingwa Spidi 360

KASI ya Yanga kwa msimu huu katika kuwania ubingwa wa Ligi Kuu ya Tanzania Bara imeonekana hakuna wa kuizuia, baada ya kuendeleza rekodi yao ya kugawa vipigo kwa kila timu ambayo wanakutana nayo mbele, baada ya jana kuwachapa African Lyon.

 

Takwimu zinaonyesha kuwa Yanga sasa inaongoza ligi hiyo ikiwa na pointi 47, ambazo ni saba zaidi ya anayefuatia (Azam FC) na pointi 17 zaidi dhidi ya Simba inayoshika nafasi ya tatu, kiasi ambacho unaweza kuifananisha kasi yao na spidi 360 katika gari zinazotumika katika mashindano.

 

Yanga ambao hawajafungwa mchezo wowote hadi sasa katika ligi hiyo waliwachapa Lyon kwa bao 1-0 kwenye Uwanja wa Sheikh Amri Abeid mkoani Arusha.

 

Shujaa wa Yanga kwenye mechi hiyo ni beki Abdallah Shaibu ‘Nin­ja’ ambaye ndiye aliyefunga bao pekee ambalo liliwapa pointi tatu na kuifanya timu hiyo iendelee kung’ang’ania usukani wa ligi.

 

Katika mechi hiyo ambayo ilikuwa na ushindani mkubwa, Yanga iliwalazimu kuvuta subira hadi dakika ya 64 kupata bao hilo ambapo Ninja kwa kichwa aki­malizia pasi iliyopigwa na Ibrahim Ajibu kutokana na mpira wa faulo.

Yanga katika pambano hilo walilazimika kuwatoa Jaffar Mo­hammed na Ramadhan Kabwili baada ya kuumia na nafasi zao kuzibwa na Deus Kaseke na Klaus Kindoki.

 

Hali ya Kabwili ilikuwa mbaya na kulazimika kutolewa uwan­jani hapo kwa gari maalum la kubebea wagonjwa (ambu­lance) kisha kuwahishwa hospitali kwa matibabu zaidi.

 

Awali, kabla ya mchezo huo baadhi ya mashabiki wa timu hiyo waliokuwa uwan­jani walionekana kutembeza bakuli kwa ajili ya kutoa fed­ha ambazo zitawasaidia timu hiyo hasa kwenye kipindi hiki ambacho inadaiwa wana ukata wa fedha.

 

Yanga walipata ushindi huo huku wakiwa hawana sehemu kubwa ya wachezaji wake pamoja na kocha wao, Mwinyi Zahera ambaye yupo Ufaransa.

Wachezaji waliokosekana ni, Thabani Kamusoko, Raphael Daud, Feisal Salum ‘Fei Toto’, Mrisho Ngassa na Papy Tsh­ishimbi.

Stori na Omary Mdose na Kennedy Lucas, Arusha

Comments are closed.