The House of Favourite Newspapers

Katika Hili, Riyama Ulitakiwa Kuchutama

NI ukweli usiopingika kwamba utakapowataja wasanii wa kike Bongo wanaofanya vizuri, jina la mwanadada Riyama Ally haliwezi kukosekana.

Binafsi namfahamu Riyama tangu kitambo kidogo, enzi hizo akiwa ndiyo kwanza anaanza kuchipukia kwenye filamu, akiwa bado kinda kisanii na kiumri! Namfahamu kuanzia kipindi hicho akiwa mahiri zaidi katika filamu za ma­jonzi na huzuni, tofauti na sasa ambapo anafiti zaidi kwenye nafasi za umcharu­ko, mwanamke wa Uswazi.

 

Binafsi nilipokutana naye kwa mara ya kwanza na kufanya naye mahojiano am­bayo yalitoka gazetini, moyoni nilijiam­bia kwamba ipo siku Riyama atakuwa msanii mkubwa sana nchini. Niliiona ‘spirit’ kubwa ndani yake, mapenzi makubwa ya sanaa, hamu ya mafanikio na nidhamu iliyotukuka, si tu katika maisha yake ya kisanii bali hata katika maisha yake halisi.

 

Miaka kadhaa imepita sasa, Riyama amepiga hatua kubwa katika sanaa, japokuwa mimi niliamini kwamba atakuja kung’ara sana kwenye ‘scene’ za majonzi, mambo yamebadilika na anaonekana kung’ara zaidi kwenye nafasi za umapepe, mcharuko, maneno mengi na kuchambana!

 

Yote kwa yote, Riyama hivi sasa ni msanii mkubwa na bila unafiki nakiri kwamba anaweza kuwa miongoni mwa wasanii wachache wa kike ambao wanakamua kisawasawa, ukita­zama filamu kumi za Kibongo, unaweza kukuta tano au sita Riyama yupo ndani yake! Hata hivyo, kuna jambo ambalo limetokea siku chache zilizopita likimhusisha mwanadada huyo na ama kwa hakika ameonesha kile ambacho wengi hawakukitarajia kutoka kwake. Hilo limetokea katika hafla ya utoaji tuzo za Sinema Zetu zilizoandaliwa kwa mara ya kwanza tangu kuanza kusuasua kwa Bongo Muvi.

 

Kitendo cha Azam kuanzisha tu tuzo hizo, kwa mtu yeyote anayeitakia mema tasnia ya filamu nchini, ni jambo la kupongezwa sana kwa sababu sasa wasanii wetu watakuwa wakiumiza vichwa kufanya kazi bora, kila mmoja akitaka kung’ara kwenye tuzo hizo ambazo kwa mujibu wa waandaaji, zitakuwa zikitolewa kila mwaka.

 

Baada tu ya kutolewa kwa tuzo hizo, wasanii wengi walione sha kuchukizwa na kitendo cha mwanadada Wema Sepetu kuzoa tuzo mbili, ikiwemo ya mwigizaji bora wa kike. Mtego huu haukumuacha salama Riyama, naye akasikika katika vyombo vya habari akitoa mapovu ya kufa mtu, mpaka kufikia hatua ya kumwaga machozi hadharani.

Malalamiko yake ni kwamba hakupewa taarifa kwamba ameshindanishwa kwenye tuzo hizo na kwamba amekatishwa tamaa kwa sababu anaamini kwamba ana­fanya kazi kubwa sana pengine kuliko msanii mwingine yeyote wa kike. Kwa lugha nyepesi, Riyama anaamini yeye ndiye aliyes­tahili kupewa tuzo ya mwigizaji bora wa kike.

 

Waswahili wanao msemo kwamba muungwana akivuliwa nguo, huchuta­ma! Yawezekana vigezo vilivyotumika katika tuzo hizo siyo vile vilivyo­zoeleka na wengi, waandaaji ndiyo wanaojua vigezo zilivyotumika na wameshafafanua sana hili, sina haja ya kulirudia.Riyama unapaswa kufahamu kwamba hata kama unafanya kazi nzuri kiasi gani, haina maana kwamba umezifanya kwa ubora zaidi kuliko wengine.

 

Yawezekana ukawa bora kwenye eneo hili, lakini ni vizuri kutambua kwamba wapo wengine ambao pia ni bora kwenye eneo lingine, kwa hiyo ustaarabu siyo kuanza kutimua mbio ukilalama kila kona ilihali nguo imeku­dondoka, waungwana huchutama kwanza.

 

Tuzo zenyewe ndiyo kwanza zimeanza, sasa ukishaanza ‘uswahili’ kama huo unaouonesha, eti ukitaka uombwe radhi na waandaaji, unafikiri zikija tuzo nyingine itakuwaje? Hivi ungeshinda hiyo tuzo kweli un­geikataa kwa sababu hukuambiwa kwamba unashindanishwa? Unaposema yasiyofaa kusemwa na msanii mkongwe kama wewe, si tu unajishusha hadhi wewe mwenyewe, bali pia unawasononesha mashabiki wako ambao miaka nenda rudi wamekuwa wakikusapoti, hata pale ambapo tuzo hazikuwepo.

HASH POWER.

Comments are closed.