The House of Favourite Newspapers

Kelvin Du Rant Mtoto Anayetisha NBA

Nyota wa Cavs, Le Bron James akiwa hoi baada ya mechi.

 

WABISHI Golden State wamefanya mambo makubwa tena baada ya kufanikiwa kutwaa ubingwa wa NBA, baada ya kuwachapa Cleveland Cavaliers, kwenye michezo 4-0 ya fainali.

 

Huu ni ubingwa wa pili mfululizo kwa wanaume hao, lakini ukiwa ubingwa wao wa tatu kati ya minne ya hivi karibuni, hakika wanastahili pongezi.

 

Lakini pamoja na timu hiyo kutwaa ubingwa huo wa NBA, mwanaume Kevin Durant naye alifanya maajabu tena baada ya kufanikiwa kutwaa tuzo ya MVP.

Mwanaume Kevin Durant

Tuzo hii ni sawa na kuiita Mchezaji Bora wa Fainali za NBA, au Mchezaji Bora wa NBA kwa mwaka husika na Durant amewafunika wote huku akiiongoza timu yake kutwaa ubingwa huo muhimu mwaka huu.

 

Durant mwenye urefu wa futi sita na inchi 11, alifanya kazi kubwa kwenye fainali za mwaka huu kama alivyofanya mwaka jana.

 

“Ni suala la safari ya msimu mzima, kuamka kila siku kwenda kufanya kazi ukiwa na timu bora kama hii ni jambo zuri na linalovutia.

 

“Mazingira ya timu hii yanakufanya unaonyesha kiwango cha hali ya juu, kila mmoja ana uwezo wa hali ya juu kwenye timu hii ndiyo maana tunafanikiwa,” alisema staa huyo.

 

Durant kwenye fainali ya mwaka huu alikuwa na wastani wa pointi 28.7, kwenye kila mchezo, alikuwa na rebaundi 10.7 na pasi za pointi 7.5, akionekana kuwa kati ya wachezaji muhimu kwenye NBA.

Kwenye mchezo wa tatu wa fainali, Durant alionyesha kiwango cha juu kwenye mchezo huo dhidi ya Cavaliers kwani alifanikiwa kufunga pointi 43, zikiwemo 3-pointer ya dakika ya mwisho kabisa kwenye mchezo huo.

 

Stephen Curry, ambaye mwanzo alionekana kuwa kwenye kasi nzuri ya kuchukua tuzo hii yeye wastani wake wa juu kabisa kwenye michezo ya NBA msimu huu zilikuwa pointi 37, ambapo pia alifunga 3-pointers mbili kwenye mchezo wa nne.

“KD alikuwa na miaka miwili bora sana, kwenye michezo ya fainali na naamini kuwa alikuwa anastahili tuzo hii, hakika mimi nitaendelea kuwa shabiki wake mkubwa kwenye kipindi changu chote cha NBA.

“Nafikiri tumefanikiwa kama timu, suala la tuzo ni muhimu kwa kila mchezaji lakini huwa halilazimishwi,” alisema Curry.

 

Kura za MVP kati ya Curry na Durrant zilikuwa 7-4, hali ambayo ilimfanya Durrant kufurahia wakati alipotangazwa kuwa mshindi wa tuzo hiyo.

“Hii ina maana gani? Hii ina maana gani? Tumeshinda ubingwa wa NBA mara mbili, sidhani kama kila mmoja anaweza kufurahi kama sisi, ninafuraha kwa kuwa tumecheza pamoja na kutwaa ubingwa huu pamoja.

 

“Jambo la msingi ni timu, timu imepata mafanikio, nami timu yetu na siyo jambo binafsi kwanza, tuzo imekuja kwa wakati muafaka,” alisema Durant.

Durant amekuwa mchezaji wa 11 kutwaa tuzo hiyo mara mbili, akiwa anaungana na mastaa wengine Michael Jordan, Magic Johnson, Shaquille O’Neal, Tim Duncan na James ambao walitwaa tuzo hiyo mara tatu, waliotwaa mara mbili ni Kobe Bryant, Larry Bird, Hakeem Olajuwon, Willis Reed na Kareem Abdul-Jabbar.

Mwaka jana, staa huyo alifanikiwa kutwaa tuzo hiyo ya MVP kwa wastani mzuri wa pointi 35.2, rebaundi 8.2, pasi za pointi 5.4.

Kwa msimu huo, Durant alifunga pointi 30 na zaidi kwenye michezo mitano ya fainali, lakini mwaka huu ameonekana kupata ushirikiano mkubwa zaidi wa wenzake.

“Kiwango cha kucheza kama timu kimeongezeka, kila siku mambo yanakuwa tofauti, naamini hata msimu ujao tunaweza kufanya vizuri kuliko msimu huu.

Kabla hajajiunga na Warriors, Durant alikuwa amefanikiwa kucheza fainali ya NBA mara moja tu kwenye kipindi cha miaka tisa ambacho amecheza NBA huku nyuma.

Aliwahi kupoteza tuzo hiyo kwa LeBron James mara moja mwaka 2012. Kwenye misimu yake miwili kuanzia alipojiunga na Golden State mwaka 2016, amefanikiwa kutwaa tuzo hiyo yenye heshima kubwa mara mbili.

Durrant ambaye ni raia wa Marekani alifanikiwa kutwaa tuzo ya Olympic mwaka 2012, 2016 na nchi hiyo, akiwa anatajwa kuwa ndiye mchezaji mahiri zaidi kwenye nchi hiyo maarufu kwa mchezo wa kikapu.

Akiwa ameanza kucheza michuano ya NBA mwaka 2007, staa huyo amefanikiwa kutwaa ubingwa wa NBA mara mbili tu ambapo mwanzo alitwaa mwaka jana na mwaka huu.

Durrant alifa-nikiwa kucheza kwenye kikosi cha Oklahoma kuanzia mwaka 2008, hadi alipoondoka hapo msimu wa 2015/ 2016 na kujiunga na Golden State.

Mshambuliaji huyo mwenye miaka 29, kuanzia akiwa na umri wa miaka 13, alilelewa na bibi yake, Barbara Davis, baada ya baba yake na mama yake kuachana na baba akamuacha kwa bibi ambaye alimlea kwa kipindi kirefu.

Comments are closed.