KIMENUKA! NDOA YA PILI YA SIRI YA Z-ANTO MAJANGA YAMKUTA
MWANAMUZIKI wa Bongo Fleva, Ally Mohamed Ahmad ‘Z-Anto’ hivi karibuni alikwaa skendo baada ya kudaiwa kuoa mke mwingine (wa pili) kwa siri huku mke mkubwa aliyejulikana kwa jina la Sara akichachamaa, hata hivyo ndoa hiyo imeibua mapya.
Habari zinadai kuwa mwanamuziki huyo hivi karibuni alifunga ndoa na dada wa msanii wa filamu, Wastara Juma aitwaye Naima huku mke mkubwa akiwa hajui, jambo ambalo ni kinyume na utaratibu wa Dini ya Kiislamu.
“Niwaambie tu kwamba hivi karibuni Z-Anto alifunga ndoa ya siri bila kumwambia mkewe ambapo amemuoa dada yake Wastara anayejulikana kwa jina la Naima, mke mkubwa akazifuma picha ndiyo siri ikafichuka.
“Umetokea ugomvi mkubwa kati ya Z-Anto na mkewe huyo kwa sababu hakumwambia kwamba anaoa mke wa pili hivyo mwanamama huyo anaumia sana na anamlaumu Wastara kwamba yeye ndiye aliyemkuwadia mumewe kwa dada yake hivyo anafanya utaratibu aende Bakwata kumshtaki mumewe,” alidai mtoa habari aliyehudhuria ndoa hiyo.
MKE ACHACHAMAA!
Akizungumza na Ijumaa Wikienda, mke wa Z-Anto alisema alikuwa anakuta meseji kwenye simu ambazo mumewe huyo alikuwa akiwasiliana na huyo Naima akawa anamuuliza lakini anakuwa mkali, baadaye aligundua kuwa walishafunga ndoa.
Baada ya hapo maelewano nyumbani yakawa ‘ziro’ hivyo yeye akiwa ni mwanamke anayejitambua wala haoni shida, utafuata taratibu za ndoa kisha kuyaacha maisha yake yaendelee.
Z-ANTO ANASEMAJE?
Baada ya gazeti hili kupata habari hizo na mkewe kutoa yake ya moyoni, wanahabari wetu walimtafuta Z-Anto ambapo alifunguka kuwa habari hizo hazina ukweli.
“Niwaambie tu kwamba hizo habari za mimi kuoa hazina ukweli, mimi na mke wangu tuko vizuri kabisa hatuna tatizo ila kama anasema ameenda Bakwata mimi ndio kwanza nawasikia nyie.
“Ningekuwa nimeoa ningeweka wazi tu lakini hakuna kitu kama hicho, kuhusu kuwa karibu na familia ya Wastara ni kwamba nilianza urafiki na familia hii kama miaka 10 iliyopita, nilikuwa namfanyia dua mume wa Wastara marehemu Juma Kilowoko ‘Sajuki’ alipokuwa anaumwa,” alisema Z-Anto.
Kuhusu picha zake na Naima za ndoa zilizosambaa kwenye mitandao, msanii huyo alisema kuna kitu walichokuwa wanakifanya kuhusiana na sanaa ambacho kwa sasa hawezi kukiweka wazi.
MSIKIE NAIMA
Dada wa Wastara, Naima alipoulizwa kuhusiana na hilo na picha za ndoa yake na Z-Anto zilizosambaa mitandaoni alikuwa na haya ya kusema;
“Jamani mimi nina mume wangu, sijafunga ndoa na Z-Anto, zile picha nilienda kupiga yeye akiwa ni msimamizi tu wa harusi nyingine ya mtu lakini siyo ndoa yangu, ingekuwa ndoa ningesema maana ni jambo la heri huwezi kuficha.”
NENO LA MHARIRI
Kila mmoja amekataa kufungwa kwa ndoa hiyo, Ijumaa Wikienda bado linausaka ukweli na iwapo litaubaini kwa mapana zaidi litarudi tena kueleza kwa undani.
Comments are closed.