The House of Favourite Newspapers

KISA DENTI CHUO KIKUU… BODABODA APELEKWA KUZIMU!

MOROGORO: Kijana mmoja dereva wa bodaboda ambaye jina lake halikufahamika mara moja anayekadiriwa kuwa na umri wa miaka 20, amepokea kichapo kutoka kwa wananchi wenye hasira kali wakimshutumu kumpora simu denti wa kike wa Chuo Kikuu Cha Waislam kilichopo Msamvu mkoani hapa ambapo kichapo hicho kimempeleka kuzimu.  

 

Tukio hilo lilitokea hivi karibuni maeneo ya lpo lpo, Modeko Kata ya Mazimbu ambapo Kamanda wa OFM alifika eneo la tukio na kushuhudia wananchi wenye hasira kali wakimgombea bodaboda huyo kama mpira wa kona hadi kufikia hatua ya kumtoa uhai (kumpeleka kuzimu).

 

Baada ya muda polisi walifika eneo la tukio na kulitawanya kundi hilo la watu ambapo walimuokoa bodaboda huyo huku wakiwashikilia wananchi wanne kwa kosa la kujichukulia sheria mkononi. Wakizungumza na Uwazi, mashuhuda waliokuwepo kwenye tukio hilo walisema kuwa, wezi hao ni wale wanaopora simu na mabegi kwa kutumia bodaboda nyakati za usiku.

“Tukio lenyewe limetokea majira ya saa 2 usiku ambapo denti huyu alikuwa amevaa hijabu anatembea huku akiongea na simu ghafla bodaboda aliyekuwa amempakia mwenzake walimpitia kama kipanga na kumpora simu yake. “Denti alipaza sauti akiangua kilio hivyo bodaboda wa eneo hili la Hedema waliposikia wakawafukuzia na kufanikiwa kuwakamata eneo la lpo lpo,” alisema Ally.

 

Shuhuda mwingine aliyejitambulisha kwa jina la Abel alisema waliona bodaboda zikitokea airport zikifukuzana, zilipofika kona ya lpo lpo ile ya mbele ikaanguka baada ya kutitia kwenye dimbwi la mchanga, yule wa nyuma akaruka na kukimbia hivyo akamuacha mwenzake akishindwa kujinasua baada ya bodaboda yake kumlalia kwa juu.

“Walipofika wale wengine waliokuwa wakiwafukuzia, wakaanza kumshushia kichapo wakidai wamempora simu denti wa Chuo cha Waislam, wananchi wakaongezeka na kuanza kumpiga kichwani kwa mawe na mateke,” alisema Abel. Hata hivyo, bodaboda huyo alipofikishwa Hospital ya Rufaa ya Mkoa wa Morogoro kupatiwa matibabu alikata roho akiwa mapokezi.

STORI: EDUNSTAN SHEKIDELE, UWAZI

Comments are closed.