RAIS John Magufuli leo Julai 6, 2020, amewaapisha viongozi mbalimbali Ikulu jijini Dodoma.
Katika uapisho huo Mkuu wa Mkoa wa Pwani, Mhandisi, Evarist Ndikilo, ambaye ni Mwenyekiti wa Wakuu wa Mikoa nchini, amewataka wakuu wa mikoa pamoja na viongozi wengine kutatua kero zilizo ndani ya uwezo wao na sio kumsubiri rais afanye ziara na kukutana nazo.
”Pamoja na maelekezo mengi unayotupa lakini kuna changamoto ya kero na malalamiko ya wananchi, na mara ya nyingi umekuwa ukikutana na kero hizo na muda mwingine unatumia muda wako kuzitatua wakati nyingi zipo ndani ya uwezo wetu hivyo nitoe rai kwa viongozi tuzitatue kero hizo.
“Kwa Wakuu wa Mikoa wateule tunawakaribisha. Mara nyingi Mheshimiwa Rais umekuwa ukitatua changamoto zilizo ndani ya uwezo wetu, hii siyo sawa. Haipendezi ukija kutatua changamoto za level (kiwango) ya kijiji. Tutakusaidia,” amesema Ndikilo.
Aidha ameongeza kuwa, ”Nichukue fursa hii kutoa rai kwa wakuu wa mikoa na viongozi wengine wa ngazi zote tusisubirti changamoto za kijiji zije zitatuliwe na Rais, makamu au Waziri Mkuu.”
Amewataka viongozi wote kumsaidia rais kwa sababu pengine ana kazi nyingi zaidi za kufanya kwa ajili ya Watanzania.