The House of Favourite Newspapers

Maalim Seif Akutana na Watendaji Wenye Ulemavu Zanzibar.

0

MAKAMU wa kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad Janauari 19 amefanya Ziara katika Idara ya Watu wenye ulemavu , Idara ambayo ipo chini ya ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar.

 

Lengo la ziara hiyo ni kukutana na watendaji wa Ofisi, kujua Changamoto zao na kubadilishana mawazo.

Mkurugenzi wa Idara hio Bi.Abeda Rashid Abdallah amesema miongoni mwa majukumu yao Idara ni kusimamia upatikanaji wa haki na usawa kwa watu wenye ulemavu pamoja na kusaidia na kusimamia Mikataba ya watu wenye ulemavu.

 

Bi. Abeda amesema mpaka kufikia sasa Idara yao imeshafika mpaka ngazi ya shehia na nahii ni kwaajili ya kusaidia utambuzi wa watu wenye ulemavu katika ngazi za mitaa na matatizo yao ili kuweza kuwasaidia.

Mkurugenzi Abeda amesema kwasasa wanapigania kujua idadi ya walemavu wote, wanatoa elimu ya Uzazi kwa watu wenye ulemavu pamoja na kutoa misaada ya vifaa.

 

Akifafanua katika hilo amesema; ‘’Database yetu Jumuishi inaonesha mpaka sasa tuna Wananchi 8330 ambao wana ulemavu, lakini tuna zaidi ya walemavu 1267 Zanzibar ambao tayari tumeshawapatia vifaa mbalimbali kama vile viti vya walemavu, magongo na hata lotion kwaajili ya walemavu wa ngozi’’.

 

Akielezea Changamoto zao Mkurugenzi amesema katika majengo mengi ya taasisi sio rafiki kwa walemavu jambo ambalo linawafanya walemavu kushindwa kuzifikia huduma.

 

Mkurugenzi Abeda amesema Idara ina mfuko wa watu wenye ulemavu ambao hutumia pia kukopeshana na mpaka sasa walemavu 85 wameshanufaika na mfuko huo ila changamoto ni kwamba ni wagumu wa kurudisha fedha hizo nakudai ni mali ya serikali hivyo zinafaa kuwanufaisha wao nasio kuzirejesha.

 

Aidha Mkurugenzi amesema wapo baadhi ya walemavu ambao wanaombaomba mabarabarani jambo ambalo sio zuri kwani tayari walishawafikia na kuwataka wafike ofisini kujiorodhesha nakuona namna yakuwasaidia lakini imebainika upo mtandao wa watu hao kutumika kuomba ikiwa ni kama ajira na kuwanufaisha watu wengine ambao wanawafadhili.

 

Mkuu wa Wilaya ya Mjini Unguja Mh. Rashid Simai Msaraka amesema yeye yupo tayari kushirikiana na Idara ya watu wenye ulemavu pamoja na kusaidiana katika kutatua kesi za uzalilishaji zinazowakuta, hivyo muda wowote watakapomuhitaji wasisite kuwasiliana nae.

Makamu wa kwanza wa Rais Maalim Seif amesema jamii haipaswi kuwadharau wala kuwatenga walemavu kwani yoyote kati yetu ni mlemavu mtarajiwa.

 

Maalim amesisitiza kwa kusema; ‘’Katiba yetu ya Zanzibar inakataa ubaguzi wa aina yoyote ile, hivyo nikosa kuwabagua walemavu, Walemavu wanastahiki kuheshimiwa nakupewa haki zao zote’’.

 

Pia inahitajika elimu kwa jamii juu ya ulemavu kwani wapo wanaodhani kuzaa mtoto mwenye ulemavu ni mikosi au laana hivyo kupelekea kuwaficha watoto hao na kuwakosesha haki zao za msingi katika jamii kama raia amesema Maalim.

 

Makamu ameeleza kwamba ipo haja ya majengo yote ya biashara au yakutoa huduma yoyote yawape vipaombele Walemavu katika kujenga miundo mbinu ya kuwasaidia nao kufikia huduma hizo.

 

Maalim amemuagiza Mkuu wa Wilaya ya Mjini Mh. Msaraka kuwadhibiti wale wote wanaowatumia walemavu kuomba pesa mabarabarani kwaajili ya kuwanufaisha wao na kuwafanya kama kitega uchumi.

Amesisitiza kwamba zipo taarifa kuna watu wanawachukua walemavu na kuwaleta Zanzibar, Maalim amesema kwamba hakatazwi mgeni kuja Zanzibar ila sio kuja kuombaomba, hivyo ni kuwadhalilisha walemavu na jambo hilo halipaswi kuvumiliwa.

 

Maalim amemalizia kwa kusema wapo walemavu ambao wanashiriki michezo ya kitaifa au kimataifa nakurudi na medali nyumbani hivyo ipo haja Serikali kuwaita, kuwatambua na kuwapa moyo.

Leave A Reply