The House of Favourite Newspapers

Mabaamedi Wamlipua Bosi Wao Irene Uwoya

UBUYU wa leo hatujauvukia maji kutoka Zanzibar, bali tumeupata maeneo ya Magomeni-Kwa Fundikira, Dar, unaitwa ubuyu wa vimto ambapo unamung’unywa kuwa, ile baa maarufu ya staa mkali wa filamu za Kibongo, Irene Uwoya ijulikanayo kwa jina la Last Minutes imefungwa kwa madai kuwa mabaamedi wake wamegoma kwa kutolipwa mishahara miezi mitatu

 

MMOJA WA WAFANYAKAZI AFUNGUKA

Msambaza ubuyu huo ambaye alikuwa ni mmoja wa mabaamedi katika baa hiyo aliyeomba hifadhi ya jina kwa sababu ya kutotaka kuonekana mmbaya, alidai kuwa, yeye na wenzake watano waliamua kuchukua uamuzi wa kugoma kwa sababu hawajalipwa mishahara ya miezi mitatu, jambo ambalo wamelivumilia kwa kipindi chote hicho.

 

“Ukweli ni kwamba kama mtu anafahamu ubinadamu, huwezi kumwacha mwenzako akiteseka wakati amekufanyia kazi kwa kipindi hata cha mwezi mmoja bila kumlipa chochote, ukizingatia maisha ya sasa ni magumu sana mtu, mtu unavumilia hadi unachoka,” alisema mfanyakazi huyo.

Taarifa hizo zilizidi kueleza kuwa, mara kwa mara wafanyakazi hao walikuwa wakimkumbushia Uwoya juu ya madai ya stahiki zao, lakini waliishia kuambiwa kuwa watalipwa kesho ambayo haikufika.

 

WADAI KUPIGWA KALENDA

Mhudumu huyo alilieleza Ijumaa Wikienda kuwa, wamekuwa wakipigwa kalenda kila siku, jambo ambalo limekuwa likiwaumiza siku hadi siku hadi kufikia hatua ya kuamua kugoma wote.

“Siku hizi kazi hakuna, lakini hadi mtu anaamua kuacha kazi, ujue kuna tatizo kubwa,” alisema mwanadada huyo.

 

IJUMAA WIKIENDA NA MAMA KUBWA

Baada ya kupata ubuyu huo, Ijumaa Wikienda liliwatafuta wahusika ambapo wa kwanza alikuwa ni Mariam Ismail ‘Mama Kubwa’ Uchunguzi wa gazeti hili kwenye baa hiyo ulibaini kuwa, Mama Kubwa ndiye meneja ambapo alipoulizwa kuhusiana na hilo, mambo yalikuwa hivi;

 

Ijumaa Wikienda: Vipi Mariam, mzima? Siku hizi hizi baa mmeifunga?

Mariam: Kwa nini?

Ijumaa Wikienda: Nimeona kama wiki hamjafungua, lakini pia kuna malalamiko kuwa hamjawalipi wafanyakazi wenu mshahara ni miezi mitatu sasa, hilo likoje?

Mariam: Nani amekuambia? Hilo siyo kweli kabisa.

 

Ijumaa Wikienda: Ukweli ni upi sasa?

Mariam: Ni kwamba pale tumefunga kwa sababu kuna matengenezo tunafanya ya kupaongeza maana kulikuwa kumebana sana hivyo wateja wengine walikuwa wanakosa nafasi.

Ijumaa Wikienda: Mbona kuna madai kuwa mmefunga kwa sababu wafanyakazi wamegoma kwa kuwa hamjawalipa mishahara yao ya miezi mitatu?

 

Mariam: Hiyo siyo kweli kabisa itakuwa ni mfanyakazi mmoja ambaye alikuwa ana matatizo na sisi. Huyo ndiye anasambaza hizo habari za uzushi, lakini sisi tuko kwenye matengenezo.

 

UWOYA ANASEMAJE?

Baada ya kumsikia Mariam, Ijumaa Wikienda lilimtafuta Uwoya ambapo alisema kuwa yeye hana cha zaidi cha kuzungumza na kwamba maelezo ya meneja wake yanajitosheleza.

UBUYU: IMELDA MTEMA, DAR

Comments are closed.