NAMSHUKURU Mungu wa Mbinguni, kwa fadhili zake ni za milele. Amekuwa nami katika kila hatua niipigayo maishani kwangu, tangu kuzaliwa kwangu hadi sasa ninapoelekea uzeeni, hakika ni mwema na sifa zake zivume kote. Jumamosi ya wiki iliyopita, Rais wa Jamhuri nya Muungano wa Tanzania, Dk. John Pombe Magufuli alifanya mabadiliko madogo kwenye Baraza la Mawaziri, ambapo aliteua wapya, wengine kuwabadilishia wizara huku baadhi yao wakiachwa kutokana na namna ambavyo aliona inafaa.
Niwapongeze wateule na hata waliopandishwa vyeo na kuwakumbusha walioachwa kuwa uongozi ni kupokezana vijiti na kamwe huwezi kushikilia nafasi fulani kwa maisha yako yoye, haiwezekani na maisha laizima yasonge. Leo ninalo neno dogo tu ambalo nataka nitete nanyi mawaziri mlioteuliwa kushika wizara mbalimbali, mliopanda au kuhamishwa wizara na husasan wale wapya ambao ni mara yao ya kwanza kuongoza wizara.
Kabla sijasonga mbele, nitoe pongezi za dhati kabisa kwa Rais Dk John Pombe Magufuli kwa uteuzi aliofanya kwani amechagua ‘vichwa’ ambavyo anaamini vitaendana na kasi yake ya kuibadilisha Tanzania katika Mawaziri wapya naombeni tutete kidogo! mbio za kuinua uchumi hususan ule wa viwanda kama ilivyo falsafa yake. Pia, kwa kutenganisha baadhi ya wizara ambazo kwa mfumo huu mpya zitahudumia wananchi kwa ufanisi. Ndugu zangu mawaziri, mmepewa nafasi ambazo mnatakiwa mzitendee haki kwa kujituma katika kuwajibikia wananchi. Rais amewaamini na kuwapeni majukumu hayo akijua kabisa mtamsaidia kutimiza ndoto yake ya kuinua nchi yetu.
Sisemi haya kwa kumaanisha kwamba hamjui majukumu yenu, lakini kama kiongozi najua kabisa tatizo la kupewa madaraka makubwa huanza kujitokeza kwa kumhusika kujisahau muda mfupi tu baada ya kupewa nafasi.
Wote ni wachapa kazi, nakujua vyema Suleiman Jaffo, sina shaka na utendaji wako, Angela Jasmini Mbelwa Kairuki vilevile sina hofu na kujituma kwako, Luhaga Joelson Mpina sijasahau umakini na uwajibikaji wako pamoja na Dk. Medard Matogolo Kalemani lakini hapohapo msisahau kabisa nakumbuka mikikimikiki yako Dk. Hamis Andrea Kigwangalla.
Kangi Alfaksadi Lugola, nakumbuka mno namna ambavyo umekuwa mtetezi wa wanyonge ndani na nje ya bunge na kichwa changu kimegubikwa na kumbukumbu za utumishi wako bora mzee wangu, Kapteni George Huruma Mkuchika na hata wewe Dk. Faustine Ndungulile, hapohapo sijakusahau Dk. Marry Mwanjelwa na wengine wengi ambao mmeingia kwenye Baraza la Mawaziri. Ndugu zangu mawaziri, fanyeni kazi kwa wimo wa moyo bila kuogopa wala kumuonea mtu.
Ndugu yangu Luhaga, zile hekeheka za mazingira njoo zano huku kwenye kilimo. Hata ndugu yangu Dk. Kigwangala umakini uliokuwa nao ukiwa Naibu Waziri wa Afya, usiuache mlangoni huko ulikokwenda kwenye Maliasili na Utalii.
Chondechonde Jafo, endeleza hapohapo. Mthibitishieni rais kwamba imani yake kwenu iko sahihi kwamba hajakosea kuwaamini. Chapeni kazi na Watanzania wanategemea mabadiliko mengi kutokana na utendaji kazi wenu, simamieni mambo kwa juhudi na zaidi sana tangulizeni hekima kwa kila mlitendalo.
Achaneni kabisa na dhana ya kutumia muda mwingi kukaa ofisini. Matatizo ya wananchi hayako ofisini kwenu, wanayo kwenye makazi yao huko wanakoishi. Tokeni, nendeni mkawasikilize na kuwatimizia mahitaji yao. Kwa hili niwapongeze sana Jaffo, Dk. Kigwangalla na Mpina lakini haimaanishi kwamba wengine hawaendi kwa wananchi, lakini nafsi yangu inaridhika sana namna ambavyo watatu hao wamekuwa wakijituma kuwafikia wananchi kila mara.
Hoja yangu hapa ni kutobweteka na viti vya kunesa na kuzunguka vya maofisini kwenu, kama nilivyosema, wafikieni wananchi. Zungukeni nchi nzima, mijini na vijijini, mashambani na mistuni mkajionee kero za wakazi wa maeneo husika na bila kuchelewa tatueni migogoro na matatizo yao. Nimalizie kwa kuwapongeza tena lakini haya ni maoni tu maana mnao uhuru wa kuchagua ama myachukue maneno yangu na kuyafanyia kazi au mkaachana nayo huku mkijikita kutekeleza majukumu yenu kwa namna ambavyo mnaona inafaa.
Muhimu sisi wananchi ni kuwapa ushirikiano wa kutosha. Kitendo ambacho kitawapa nguvu na matumaini ya kufanya kazi zaidi. Ondoeni watu wote ambao mnadhani watakuwa ukuta wa kuwazuia kufanya kazi.Haijalishi kama ni ndugu, rafiki au mtumishi aliye chini ya wizara zenu.
Mwisho kabisa, shirikianeni nyinyi kwa ninyi. Mfano kama Dk. Ndungulile akiwa na shida ya ushauri unaohusiana na Wazara ya Afya na akakufuata wewe Dk. Kigwangalla, muoneshe ushirikiano wa kutosha na ukifanya hivyo utajiwekea alama iliyotukuka kwa mhusika, Watanzania na Mungu pia na asiyefanya hivyo atakuwa anajitenda na maendeleo. Jipu limepasuka na kamwe siwezi kuwa adui kwa kusema kile ninachoamini kuwa ni ukweli.
Napasua Jipu, Eric Shigongo