The House of Favourite Newspapers

Mbelgiji Ajifungia Kuwasoma Nkana

Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Aussems.

WAKATI Simba ikitarajiwa kupambana na Nkana FC ya Zambia, Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Aussems, jana mchana alitumia muda wake kuziangalia video za wapinzani wao hao.

 

Aussems, raia wa Ubelgiji, alifanya hivyo ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya kuwaondosha wapinzani wao hao na kutinga hatua ya makundi ya Ligi ya Mabingwa Afrika.

 

Simba iliyotinga hatua hiyo kwa jumla ya mabao 8-1 baada ya kuiondosha Mbabane Swallows, itaanzia ugenini kucheza na Nkana mechi itakayochezwa Desemba 14, kisha timu hizo zitarudiana jijini Dar Desemba 21, mwaka huu.

 

Mshindi wa jumla katika mchezo huo, atafuzu hatua ya makundi na atakayefungwa, ataangukia Kombe la Shirikisho Afrika kusaka nafasi ya kutinga makundi.

 

Akizungumza na Championi Jumamosi, Aussems alisema tangu mwanzo malengo yao ni kutinga hatua ya makundi ya michuano hiyo na si kitu kingine, hivyo ni lazima watumie mbinu zote kuhakikisha wanafikia malengo yao hayo.

 

“Katika michuano hii hakuna timu ya kuidharau, yeyote utakayekutana naye unatakiwa kujiandaa vizuri kumshinda. Tunashukuru tumeweza kuvuka hatua ya awali kwa ushindi mzuri, sasa tunataka kufanya hivyo katika hatua hii.

 

“Leo (jana) mchana nitatumia muda wangu kujifungia ndani kuangalia video za wapinzani wetu hao nione namna ya uchezaji wao wanapokuwa nyumbani na ugenini. Kupitia video hizo kuna kitu nitakibaini,” alisema Aussems.

Comments are closed.