The House of Favourite Newspapers

Mkandarasi wa usafirishaji umeme atakiwa kumaliza kazi ifikapo Aprili 2016

0

acb4cb83-7e8a-4b48-b4ab-950ff1496751Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani (kushoto) akisaini kitabu cha wageni katika ofisi ya Mkuu wa mkoa wa Dodoma kabla ya kuanza ziara ya kukagua miundombinu ya usafirishaji umeme, miradi ya umeme vijijini pamoja na shughuli za uchimbaji wa madini mkoani humo. Kulia ni Mkuu wa mkoa wa Dodoma, Chiku Galawa.

a22aeb8e-8bd3-4052-84ff-ae1501ec05f6
Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani (wa kwanza kulia) akizungumza na Meneja Mradi Ujenzi wa vituo vya kupoozea umeme katika mradi wa Miundombinu ya Usafirishaji Umeme wa Kilovolti 400 kutoka Iringa hadi Shinyanga, Mhandisi James Mtei (katikati) mara baada kukagua ujenzi wa kituo cha kupoozea umeme kilichopo eneo la Zuzu mkoani Dodoma.afc562ae-124e-4c2c-8dfe-1f7d327efc17Sehemu ya mitambo katika kituo cha kupoozea umeme kilichopo eneo la Zuzu mkoani Dodoma. Ujenzi wa kituo hicho ni sehemu ya utekelezaji mradi wa ujenzi wa miundombinu ya usafirishaji umeme wa kilovolti 400 kutoka Iringa hadi Shinyanga unaotarajiwa kukamilika mwezi Aprili mwaka huu. Kituo kinajengwa na kampuni ya GSE&C na Hyosung kutoka Korea.

Kampuni ya Joti structures inayojenga miundombinu ya usafirishaji umeme wa msongo wa kilovolti 400 kutoka Dodoma hadi Singida imetakiwa kukamilisha ujenzi wa miundombinu hiyo ifikapo mwezi Aprili mwaka huu kama mkataba unavyoelekeza.

Agizo hilo limetolewa na Naibu Waziri wa Nishati na Madini, Dkt. Medard Kalemani wakati alipofanya ziara ya kikazi mkoani Dodoma ili kukagua miundombinu ya usafirishaji umeme, miradi ya umeme vijijini pamoja na shughuli za uchimbaji wa madini.

Alitoa agizo hilo baada ya Meneja anayesimamia Mradi huo kutoka Shirika la Umeme nchini (TANESCO), Mhandisi Oscar Kanyama kumueleza kuwa mkandarasi huyo amekamilisha ujenzi wa nguzo (transmission tower) kwa asilimia 30 tu toka alipokabidhiwa kazi hiyo mwaka 2013.

“Mkandarasi alianza kazi Novemba 2013 na anatakiwa akamilishe tarehe 20 Aprili 2016 na hadi kufikia Desemba mwaka 2015 ilibidi awe ameshaanza kuvuta nyaya kutoka Dodoma hadi Singida lakini mpaka sasa hajaanza,” alisema Mhandisi Kanyama.

Naibu Waziri aliongeza kuwa mkandarasi huyo asipokamilisha kazi ndani ya muda uliopangwa atalazimika kulipa gharama ambazo serikali itakuwa imeingia kutokana na mkandarasi huyo kuchelewesha mradi husika na kupelekwa mahakamani.

“Serikali imeshalipa asilimia 60 ya gharama zinazotakiwa ili kukamilisha mradi huu lakini huyu mkandarasi amekamilisha kazi kwa asilimia 30 tu, hii haikubaliki, hatutamvumilia mtu yeyote anayekwamisha juhudi za usambazaji umeme nchini, awe mkandarasi au wasimamizi kutoka serikalini wanaosimamia miradi hii,” alisema Dkt. Kalemani.

Kwa upande wake, Meneja Mkazi wa kampuni ya Joti Structures, D.N. Charjee alimueleza Naibu Waziri kuwa watakamilisha kazi husika ndani ya muda uliopangwa kama ilivyo ndani ya mkataba na kwamba asilimia 15 iliyobaki ya vifaa vinavyohitajika ili kukamilisha kazi hiyo vitafika tarehe 12 Januari 2015.

  1. Wakati huohuo Naibu waziri amepiga marufuku shughuli za uchimbaji wa madini ya ujenzi ndani ya mita 30 kutoka katika korongo la Ihumwa mkoani Dodoma kwa kuwa zimekuwa zikiathiri uwepo wa maji katika kata ya Ihumwa na sehemu nyingine zinazotegemea maji hayo kwa shughuli mbalimbali.

Baada ya kuona athari za uharibifu wa mazingira katika korongo hilo, Naibu Waziri alimwagiza Kamishna Msaidizi wa Madini Kanda ya Kati, Sostenes Massola kuhakikisha kwamba agizo hilo linafanyiwa kazi kwani wananchi wengi katika kata hiyo wanaopata kipato kutokana na kilimo cha umwagiliaji wanaathirika.

“Sheria ya mazingira hairuhusu kuharibu vyanzo vya maji, kama kuna uchimbaji wa madini ya ujenzi , Kamishna Msaidizi lazima uhakikishe kwamba haufanyiki ndani ya mita 30 kutoka kwenye mito na wachimbaji lazima wawe na vibali,” alisema Dkt. Kalemani.

Leave A Reply