The House of Favourite Newspapers

Mkude: Pointi za Azam Zitatupa Ubingwa

Kikosi cha timu ya Simba.

KIUNGO wa Simba, Jonas Mkude, amefunguka kuwa ni muhimu kwao kuifunga timu ambayo wako nayo katika harakati ya kuwania ubingwa, hivyo Azam FC ijipange baada ya kufanikiwa kuifunga Yanga.

 

Simba ilifanikiwa kuifunga Yanga, wikiendi iliyopita ambapo wapinzani wao hao ndiyo vinara wa Ligi Kuu Bara huku leo Ijumaa Simba wakitarajiwa kuwa uwanjani kuivaa Azam FC.

Jonas Mkude.

Timu hizo zitakipiga kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam ukiwa ni mchezo wao wa kwanza kukutana msimu huu katika ligi kuu.

 

Akizungumza na Championi Ijumaa, Mkude alisema wamejipanga kuondoka na ushindi sababu ni timu ambayo wapo nayo kwenye vita ya kuwania ubingwa, hivyo lazima waifunge kama ilivyokuwa kwa Yanga.

 

“Unajua kwa sasa ushindani umekuwa mkubwa sisi tunaenda kuvaana na Azam ni lazima tujitume kwa bidii kupata pointi mbele yao sababu wao nao wako kwenye mbio za kutetea ubingwa na sisi tunatakiwa kuwashinda kama tulivyofanya kwa Yanga,” alisema Mkude.

 

Simba inaingia katika mchezo dhidi ya Azam FC ikiwa na viporo vya mechi nane hadi sasa kwenye ligi hiyo baada ya kucheza mechi 17 na kupata pointi 42, Yanga ikiwa na michezo 25 na pointi 61, Azam ina mechi 24 na pointi 50.

 

Wakati huohuo, Kocha Mkuu wa Simba, Patrick Aussems amesema: “Malengo yetu ni kuona tunafanikiwa kutetea ubingwa wa msimu huu lakini huwezi kufanikiwa kama hujawafunga Azam, tunaangalia mchezo huo katika akili nyingine ili tuweze kufikia malengo.”

Comments are closed.