Museveni Aidhinisha Sheria Kuondoa Kikomo Umri Wa Rais
RAIS wa Uganda, Yoweri Museveni, ameidhinisha mswada unaoondoa kikomo cha umri kwa wagombea urais nchini humo, hatua inayompa nafasi ya kuwania tena urais mwaka 2021. Mswada huo pia unarejesha rais kuongoza kwa mihula miwili pekee ya miaka mitano kila mmoja na kwa kuwa sheria hiyo itaanza kutekelezwa sasa, Museveni anaweza akaongoza taifa hilo hadi 2031.
Kwa mujibu wa gazeti la Daily Monitor la Uganda, Katibu wa Rais, Bi Linda Nabusayi, amesema Museveni alitia saini mswada huo kuwa sheria Desemba 27 mwaka jana na kisha akatuma waraka Desemba 29. Sheria ya awali ilikuwa inamzuia mgombea kuwania urais baada ya kutimiza umri wa miaka 75 ambapo Museveni kwa sasa ana miaka 73.
Hatua ya rais huyo kuidhinisha mswada huo imetoka wakati ambao amekuwa akihimizwa na viongozi wa kidini na wanaharakati wa kisiasa kutouidhinisha.
Bunge liliidhinishwa mswada huo mnamo Desemba 10 kwa zaidi ya theluthi mbili ya wabunge waliohudhuria kikao ambapo wabunge 317 waliunga mkono na 97 wakapinga.
Comments are closed.