The House of Favourite Newspapers

Mwanza: Mwanamke Akamatwa na Shehena ya Bangi

Kamanda Msangi.

KAMANDA wa Polisi Mkoa wa Mwanza, DCP Ahmed Msangi amesema mtuhumiwa Mwanamke Asha Jeremiah (32), amekamatwa kwa kosa la kukutwa na gunia la bangi na kwamba atafikishwa mahakamani baada ya upelelezi kukamilika.

Kamanda Msangi amesema Jeshi hilo linaendelea na upepelezi pamoja na msako katika maeneo mbalimbali ya visiwa vya Wilayani Ukerewe na pindi upelelezi utakapokamilika Asha atafikishwa mahakamani.

Asha mkazi wa Kisiwa cha Lyegoba, anashikiliwa kwa kosa la kupatikana na bangi ikiwa kwenye gunia moja lililojaa, maboksi matatu yaliyojaa bhangi na misokoto ya bhangi 371, vyote vikikadiriwa kuwa na uzito wa kilogramu kati ya 35 hadi 50, jambo ambalo ni kinyume cha sheria.

Msangi ameeleza kuwa askari walipokea taarifa kutoka kwa raia wema juu ya uwepo wa mtu anayejihusisha na uuzaji wa bangi katika Kisiwa cha Lyegoba na baada ya ufuatiliaji ndipo walifanikiwa kumkamata mtuhumiwa akiwa na bangi hiyo.

Aidha, Msangi ametoa wito kwa wananchi wa mkoa wa Mwanza kuacha kujihusisha na vitendo vilivyo kinyume cha sheria na kuendelea kutoa ushirikiano kwa jeshi hilo ili kufanikisha kukamatwa kwa waharifu.

Comments are closed.