MSTAHIKI Meya wa Jiji la Dar es Salaam, Isaya Mwita, amezitaka halmashauri zote katika jiji lake kuajiri watumishi watakaozika watu ambao watabainika kuwa hawana ndugu.
Aliyasema hayo jana katika kikao cha robo ya pili ya Baraza la Madiwani wa Jiji la Dar es Salaam ambapo amewaeleza madiwani hao kuwa hadi sasa jiji limeshanunua gari na mahitaji mengine ya kuhifadhia miili hiyo pindi inapotokea na kwamba changamoto iliyopo ni watu ambao watashirikiana kutekeleza jukumu hilo.
“Tulikubaliana jambo hili lifanyike kwenye halmashauri zetu, lakini hadi sasa Kinondoni pekee ndiyo wametimiza agizo hili, sasa ninaagiza tena halmashauri nyingine za jiji hili kuajiri watu hao,” amesema Mwita.
“Hivyo marehemu wanapokuwa wamekaa muda mrefu wanalazimika kuzikwa na jiji, tulikubali kuchangia usafiri, dawa na sanda,” amesema.
Amefafanua kuwa watu wasiokuwa na ndugu wanapokufa na kukaa hospitalini zaidi ya siku 20, jiji linalazimika kuwazika hivyo wapo ambao wanazikwa kwenye halmashauri mbalimbali.
Comments are closed.