KIUNGO wa Yanga, Thabani Kamusoko raia wa Zimbabwe amefunguka kuwa anafurahia baada ya kupona kwa jeraha lake la goti na kuweza kurejea uwanjani kwa ajili ya kuitumikia timu hiyo inayonolewa na Mzambia George Lwandanima.
Mbali na Kamusoko, pia wachezaji wengine wawili Donald Ngoma na Amissi Tambwe wanatarajiwa kurejea uwanjani hivi karibuni.
Hawa wanarejea kipindi ambacho timu yao inajiandaa na mchezo wa Ligi Kuu Tanzania Bara dhidi ya Simba utakapigwa Machi 7 kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar.
Kwa muda mrefu Kamusoko nyota wa zamani wa FC Platinum ya Zimbabwe alikosekana kwenye kikosi hicho kutokana na kuwa nje akijiuguza jeraha hilo ambalo alilipata zaidi ya miezi minne iliyopita.
Hadi sasa kiungo huyo tayari amerejea ndani ya kikosi cha kwanza cha timu hiyo na tayari ameshafanikiwa kucheza michezo miwili ule wa ligi kuu dhidi ya Kagera Sugar na Ligi ya Mabingwa Afrika dhidi ya Township Rollers ya Botswana ambapo mechi zote hizo hakufanikiwa kumaliza dakika 90.
“Nilikuwa na wakati mgumu nilipokuwa majeruhi kwa sababu hii ni kazi yangu, hivyo ilikuwa inaniuma kuona nipo nje, ni vizuri nimepata nafuu na nina furaha kurudi uwanjani tena,” aliandika Kamusoko kwenye Mtandao wa Instagram.
Wakati Kamusoko akirejea na kuanza kuitumikia Yanga kikamilifu, wachezaji Amissi Tambwe na Donald Ngoma nao hivi karibuni wanatarajiwa kurejea tena uwanjani kuitumikia timu hiyo.
Kama Tambwe na Ngoma wakirejea uwanjani basi itakuwa mbaya sana kwa upande wa Simba ambao walikuwa wanatarajia kuvaana na Yanga ambayo haina wachezaji wengi wenye uzoefu.
Comments are closed.