Nyumba ya Karne ya 18 Inauzwa kwa Paundi 110,000, Iko Njiapanda Uingereza
NYUMBA ndogo iliyojengwa karne ya 18 ikiwa na chumba kimoja cha kulala na sebule ghorofani na maliwato sehemu ya chini, inauzwa kwa Paundi 110,000 (Sh. milioni 295) katika kijiji cha Stanton Drew, Somerset, Uingereza.
Nyumba hiyo ya umbo la mviringo iko katika njiapanda ya mabarabara mawili, japokuwa haina eneo la kuegesha gari lakini kando ya barabara hizo kuna sehemu ya maegesho. Pia eneo la jikoni lina nafasi ya kuweka meza ndogo na viti wakati ambapo sehemu ya huduma za maji pia hutumika kama maliwato.
Nyumba hiyo ambayo ilijengwa mnamo karne ya 18 ilikuwa ikitumiwa na familia moja iliyokuwa inakusanya ushuru wa matumizi ya barabara hizo ambapo kulikuwa na kibanda cha mtu aliyekuwa anakusanya fedha hizo kutoka kwa madereva.
Nyumba hiyo ambayo imeezekwa kwa nyasi iko karibu sana na kijiji cha Chew Magna ambapo kuna shule ya msingi, baa, kanisa na ukumbi wa kijiji, duka kubwa la vyakula na vifaa (supermarket), posta na benki.
Nyumba hiyo ilitumikia katika kituo cha ushuru hadi mwishoni mwa miaka ya 1870 na baadaye kuwa makazi ya kawaida hadi sasa. Mmiliki wa nyumba hiyo amekuwa nayo tangu mwaka 2000 na sasa anataka mtu mwingine ainunue na kufurahia mazingira yake.
Comments are closed.