Polepole Awazungumzia Viongozi Wa Dini
KATIBU wa Itikadi na Uenezi wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) Humphrey Polepole amesema Askofu Zakaria Kakobe na viongozi wengine wa dini hawajazuiwa kuongea na kwamba wako huru kutoa maoni yao.
Polepole alisema hayo jana wakati akihojiwa na kituo kimoja cha televisheni aliposema hakuna mtu ambaye ametishwa kwa kusema ukweli juu ya jambo fulani ambalo huenda lipo au linatokea Tanzania.
“Hakuna mtu amezuiliwa kuongea ukweli Tanzania, hakuna mtu ametishwa kwa kusema ukweli na hasa katika uongozi wa awamu ya tano chini ya Rais Dkt. John Pombe Magufuli. Anayesema kuna mtu kazuiwa kuzungumza atakuwa na matatizo, ila nachofahamu ni kwamba mtu kuzungumza lugha ya matusi, kwa mujibu wa katiba yetu na sheria zetu ni makosa,” alisema Polepole
Polepole aliendelea kusisitiza kuwa viongozi hao wa dini wapo wazi na huru kusema chochote kile kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Jana Katibu Mkuu wa Wizara ya Mambo ya Ndani, Meja Jenerali Mst. Projest Rwegasira, ilitoa onyo na kuwataka viongozi wa jumuiya za kidini kutotumia mahubiri yao ya ibada kwa kufanya uchambuzi wa masuala ya siasa.
Comments are closed.