MTANGAZAJI wa kimataifa kutoka Idhaa ya Kiswahili ya Sauti ya Amerika (VOA) ambaye ni mhariri wa idara hiyo na mtangazaji wa Kipindi cha Straight Africa Talk, Shaka Ssali juzi (Jumatano) alitembelea Ofisi za Global Publishers, Bamaga-Mwenge jijini Dar na kufanya mahojiano maalum ambapo alitoa neo la kudumisha uzalendo na kuhakikisha vijana wanapigania ndoto za kutimiza malengo yao.
Katika mahojiano hayo yaliyofanywa na chaneli namba moja ya mtandaoni ya Global TV Online, Shaka alitumia nafasi hiyo kuwataka vijana kujitoa kwa hali na mali, katika kuhakikisha wanadumisha upendo na amani huku akitumia nafasi hiyo pia kuwataka baadhi ya viongozi wa Afrika kuhakikisha wanatimiza majukumu ya kukuza na kuendeleza demokrasia na kuhudumia wananchi kwa utoshelevu bora.
Pia, Shaka Ssali ambaye atakuwa ni miongoni mwa wageni na wazungumzaji wa Tamasha la Meza ya Uzalendo, linalotarajiwa kurindima Septemba 2, 2017 kwenye Ukumbi wa Nkrumah uliopo Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, alitumia nafasi hiyo kuwataka vijana kudumisha uzalendo kwa nchi zao na zaidi sana kuhakikisha wanatimiza ndoto zao maishani, ikiwa ni pamoja na kujitolea kwa moyo wote kujenga nchi zao.
“Nimefurahi sana kutembelea Global Publishers, lakini pia nimeona namna ambavyo mnaonekana kuwa na juhudi za kupambana na maisha, tupendeni sana kudumisha uzalendo wetu, viongozi wa Afrika nao waendelee kuhakikisha wanatoa huduma stahiki kwa wananchi, pia vijana ni muhimu kupigania ndoto za maisha yetu kwa kufanya yaliyo mema, kujielemisha vya kutosha juu ya ndoto na malengo yenu, mfano mimi nasoma sana vitabu, na majarida kuhusu kazi yangu, nawapenda sana na Mungu awabariki,” alisema Shaka Ssali.
STORI| BRIGHTON MASALU| IJUMAA