The House of Favourite Newspapers

Simba Bingwa 98%

HAKUNA ubishi tena kwamba Simba imefanikiwa kubeba ubingwa wa Ligi Kuu Tanzania Bara msimu wa 2017/18 labda itokee miujiza isiyo ya kawaida. Kimahesabu, Simba wanatakiwa kupata sare mbili tu katika mechi zake tatu zilizobaki, hivyo unaweza kusema ina asilimia 98 za ubingwa.

Na Simba hii itako­saje hizo sare mbili katika mechi zake tatu zilizobaki dhidi ya Singida, Kagera na Majimaji wakati hadi sasa imecheza jumla ya mechi 27 kwenye Ligi Kuu Bara bila kupoteza hata moja?

 

Jana Simba iliichapa Ndanda FC inayopambana isishuke daraja, bao 1-0 na kufikisha pointi 65 katika msimamo wa ligi, lakini kinachowavutia watu zaidi ni kwamba timu hii ndiyo pekee katika msimamo huo ambao haijapoteza mechi.

Yanga imeshapigwa mechi mbili, Azam im­epigwa tatu. Sasa Yanga ambayo ipo katika nafasi ya tatu, inahitaji zaidi ya miujiza ili iweze kuikamata Simba. Imeachwa pointi 17 ikiwa imebakiza mechi sita ambazo zina jumla ya pointi 18. Si rahisi.

 

Na hata kama Simba ikipoteza mechi zote zilizobaki, halafu Yanga ikashinda zote, zikalingana pointi, bado itawalazimu Yanga wafanye miujiza ya kufunga angalau zaidi ya mabao matatu katika kila mechi, kitu ambazo ni nadra kutokea.

Hivyo, mashabiki wa Simba ni rahisi tu kusema kwamba waanze kushan­gilia ubingwa.

Emmanuel Okwi jana alifunga bao hilo pekee la Simba na kufikisha mabao 20, ambayo ni nusu ya ma­bao yaliyofungwa na Yanga hadi sasa kwenye ligi.

 

Pia Simba ina mabao 60 ikiwa inaongoza kwa kufunga mabao mengi zaidi katika ligi msimu huu, timu inayofuata kwa mabao mengi ni Yanga ambayo ina 40. Tofauti ya mabao 20.

Hii inaonyesha kwamba Simba imekuwa na safu imara zaidi ya ushambuliaji kuliko timu zote.

Katika mechi hiyo iliyochezwa jana kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam bao hilo la Simba lilifungwa na Mganda, Okwi katika dakika ya 43 kwa ku­piga shuti kali la mguu wa kushoto nje ya 18 na kufiki­sha mabao 20 akiendelea kuongoza katika ufungaji.

 

Katika dakika za mwan­zoni za mchezo, Ndanda ilionekana kucheza pasi nyingi huku wakitawala mpira na kulishambulia goli la Simba huku msham­buliaji wao, Omary Mponda akionekana kukosa umakini kwa kushindwa kutumia nafasi mbili za wazi kufunga mabao.

Dakika ya 23 ya mch­ezo huo, Shiza Kichuya alimanusura aifungie Simba baada ya kupiga shuti kali lililogonga mwamba wa juu na kurudi uwanjani kabla ya kuokolewa na dakika ya 20 Hemed Khoja alipewa kadi ya njano kwa kumchezea vibaya Nicholas Gyan.

 

Kikosi cha Simba kilicho­anza katika mchezo huo ni; Aishi Manula, Gyan, Asante Kwasi, James Kotei, Yusuf Mlipili, Erasto Nyoni, Jonas Mkude, Shomari Kapombe, Okwi, John Bocco na Ki­chuya.

Ndanda ; Diel Makonga, Wiliam Lucian, Ayoub Masoud, Ibrahim Job, Khoja, Jacob Massawe, Salum Minely, Majid Bakari, Mponda, Mrisho Ngassa na Tiba John.

Dakika ya 62 Simba ilifanya mabadiliko kwa kumtoa Nicholas Gyan na kuingia kinda, Rashid Juma na dakika ya 71 Asante Kwasi alitolewa na kuingia Hussen Mohamed ‘Zim­bwe’ kuchukua nafasi yake. Dakika ya 90, Okwi alitoka akaingia Laudit Mavugo.

 

Ndanda nao walifanya mabadiliko katika dakika ya 74 kwa kumtoa Mponda na kuingia Nassoro Kapama, lakini mabadiliko hayo yalionekana kumchukiza Mponda na kuonekana akirusha mikono kwenye benchi la ufundi akilalami­ka kutolewa kwake.

Ndanda imebaki katika nafasi ya pili kutoka mkiani ikiwa na pointi 23, juu yake kuna Majimaji ambayo nayo ina pointi 23. Hadi sasa timu zilizo kwenye mstari wa kushuka daraja ni Njombe Mji na Ndanda.

 

Katika michezo mingine jana, Azam ilichapwa mabao 2-1 na Stand United kwenye Uwanja wa Kam­barage, Shinyanga. Mabao ya Stand yalifungwa na Sixtus Sabilo na Ally Ally huku lile la Azam likifun­gwa na Shaban Idd.

Kagera ilitoka suluhu (sare ya bila kufungana) na Mbeya City, kama ilivy­okuwa kwa Majimaji na Mtibwa.

Azam imebaki katika nafasi ya pili ikiwa na pointi 49, lakini Yanga ina viporo vingi na kama ikishinda itakaa katika nafasi hiyo.

Omary Mdose, DSM

Comments are closed.