The House of Favourite Newspapers

SIMBA, YANGA ZAMSHINDWA TUYISENGE

WAKATI Simba na Yanga zikipambana kupata saini ya mshambuliaji Mnyarwanda, Jacques Tuyisenge, klabu ya Petro Atletico ya Angola imeweka mzigo mezani wa kiasi cha Sh.Mil.335.

 

Kwa sasa nyota huyo amekuwa akihusishwa kujiunga na klabu za mataifa tofauti zikiwemo zile za Simba na Yanga ambazo nazo zimekuwa zikimuwania tangu msimu uliopita wa Ligi Kuu Bara.

 

Tuyisenge ambaye hucheza pacha mshambuliaji wa Simba, Meddie Kagere katika kikosi cha timu ya taifa ya Rwanda ‘Amavubi’ anataka mshahara wa Sh. Mil 18. Meneja wa straika huyo, Patrick Gakumba ameliambia Spoti Xtra, kuwa kwa sasa Tuyisenge anaweza asitue katika klabu hizo kutokana na bei yake kuwa juu lakini Waangola hawamkosi. “Hakuna sehemu ambayo Tuyisenge amesaini hadi sasa.

 

Siyo huko Angola wala timu yoyote ile ambayo imekuwa ikihusishwa kumtaka, Jacques ni bado yupo Gor Mahia na anaendelea kuwepo huko na hapo Tanzania sidhani kama anaweza kuja.

 

“Mimi ninaendelea kusema kwamba kwa klabu yoyote ile ambayo inamtaka yeye Tuyisenge basi ni lazima iwe tayari kutoa kiasi cha dola laki mbili kama uhamisho wake na dola elfu nane kwa ajili ya mshahara wake.

 

Kiasi hicho kinaonekana kama kikubwa kwa huko Tanzania hivyo sidhani kwamba anaweza kuja huko,” alisema Gakumba. Hata hivyo, katibu wa Gor Mahia Judthi Nyangi amesema ; “Ni kweli tumepata ofa mezani kutoka kwa klabu ya Petro Altetico ya Angola na tuko kwenye majadiliano kama mambo yatakwenda sawa na katika hizo fedha klabu itapata asimilia 20.”

MARTHA MBOMA, na Mtanda

Comments are closed.