Katika Gazeti la Amani, kuna kolamu inayoitwa Video Review na wiki hii, video inayochambuliwa ni ngoma mpya ya Ditto aliyoipa jina la ‘Moyo Sukuma Damu’.
Sehemu ya vipande vya video hiyo
Soma mwenyewe hapa umsikie anasemaje!
Ni matumaini yangu kwamba msomaji kona hii ya Video Review uko poa.
Ni wale wenye chuki binafsi pekee ndiyo watakaoshindwa kumpongeza Ditto, kwa kazi nzuri aliyoifanya kwenye ngoma yake mpya ya Moyo Sukuma Damu, baada ya kuwa amekaa muda mrefu bila kusikika kwenye gemu la muziki wa kibongo.
Kama umepata bahati ya kuusikiliza wimbo huu, utakubaliana nami kwamba kweli jamaa ameumiza kichwa na hata ukimya wake wa muda mrefu, haukuwa bure, umekuja na mshindo mkuu.
Tukianzia kwenye suala zima la mavazi, Ditto amejitahidi kutoka kisasa, japokuwa hajafikia asilimia 100 za mavazi ya kisasa lakini kwa kiasi kikubwa amejitahidi, video queen naye amejua kwelikweli kupangilia mavazi, kuanzia pale anapoonekana akiwa chumbani, akiwa anasoma kitu kwenye faili, akiwa kwenye ‘balcony’ mpaka kwenye kipande cha mwisho anapoonekana akiwa amevaa nguo nyekundu.
Ukija kwa upande wa ubora wa picha, ipo wazi kwamba dairekta amefanya kazi ya ziada kuhakikisha ‘scene’ zote zinakuwa na mwanga wa kutosha na picha zinaonekana kwenye ubora wa hali ya juu, High Definition (HD) ambao ndiyo unaotakiwa hivi sasa katika soko la video za muziki duniani kote.
Ukiangalia video kuanzia mwanzo, huwezi kuchoka kuendelea kuitazama tena na tena, picha zinaonekana katika ubora wa hali ya juu sana, hilo pia nampongeza dairekta pamoja na Ditto mwenyewe. Ukija kwenye suala zima la location, video imerekodiwa juu ya ghorofa lililopo ufukweni na kwa kiasi kikubwa, mandhari ni mazuri mno.
Pale wanapoonekana wakiwa chumbani, unaona kweli ni chumba chenye hadhi ya juu, samani ndani zimepangiliwa vizuri na kila unachokiona, kina ubora wa hali ya juu, tofauti na ilivyokuwa mwanzo.
Dosari ndogo inayoonekana, ni kwa Ditto mwenyewe kushindwa kuuvaa uhalisia katika kipande anachoonekana akiwa amelala kitandani, daktari akimpima mapigo ya moyo. Ukimtazama Ditto, haoneshi kama kweli ni mgonjwa ambaye moyo wake unashindwa kusukuma vizuri damu kwa sababu ya maumivu ya kimapenzi, anaonekana dhahiri kwamba ni kama anaigiza.
Ukifuatilia kwa makini, kuna sehemu anaonekana kama anatabasamu hivi, jambo ambalo ni nadra kutokea kwa mgonjwa ambaye yupo mahututi. Ilitakiwa sura yake ioneshe kwamba kweli anaumwa na yupo mahututi.
Kwa upande wa video queen, nimsifu kwamba amejitahidi sana kuvaa uhalisia, hasa pale anapoonekana akibubujikwa na machozi. Hata ukiitazama video yote kuanzia mwanzo, anaonekana kweli ana maumivu makali ndani ya moyo wake, yaliyosababishwa na kuumizwa kimapenzi.
Pia ukifuatilia mtiririko mzima wa matukio, kama kuna kitu hakijamalizika vizuri. Wimbo unahusu mtu aliyeamua kuachana na mapenzi kwa sababu anaumizwa muda wote, lakini kipande hicho kinaonekana mwishoni tu mwa video hiyo ambapo Ditto analumbana na mpenzi wake lakini haioneshi mwisho wa malumbano yao, zaidi ya kuonekana mmoja amekaa upande mmoja wa ukuta na mwingine upande mwingine.
Lakini yote kwa yote, video ni kali sana, big up kwa Ditto kwa kazi nzuri.
Comments are closed.