The House of Favourite Newspapers

Vigogo Kurudishwa Yanga SC

VIGOGO wa Yanga ambao walikatwa majina yao kwenye mchakato wa uchaguzi wa viongozi wa Yanga unaotarajiwa kufanyika Mei 5, mwaka huu watarudishwa ndani ya uchaguzi endapo watakata rufaa na kupita baada ya kuondolewa kwa kutokidhi vigezo.

 

Yanga kwa sasa ipo kwenye mchakato wa kufanya uchaguzi ambapo hatua iliyopo kwa sasa ni usaili na Jumatano ya Aprili 24 mpaka Aprili 26 wanatarajia kupokea rufaa za wagombea ambao walikatwa.

Vigogo hao ambao walikatwa ni pamoja na Lucas Mashauri aliyekuwa anagombea nafasi ya mwenyekiti ambaye hakuhudhuria usaili, Samwel Lukumay ambaye alienguliwa kwa pingamizi alikuwa akigombea nafasi ya Makamu Mwenyekiti.

 

Kwa upande wa wagombea nafasi za ujumbe ni pamoja na Ally Sultan, Abdallah Chikawe, Seif Hassan ambao hawakuambatanisha nyaraka, Seko Kingo, Rodgers Gumbo, Paulina Conrad, Mkumbo Elias ambao hawana uzoefu, Siza Lyimo na Hussien Nyika waliwekewa pingamizi, Cyprian Musiba, Said Rashid, hawakuhudhuria usaili, DK Nassoro Ally alifungiwa na BMT.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Mwenyekiti wa Kamati ya Uchaguzi wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Malangwe Mchungahela, alisema kuwa rufaa itakuwa wazi kwa wagombea wote kuanzia Aprili 24 mpaka 26.

“Rufaa itafunguliwa Aprili 24 mpaka 26 na itasikilizwa kuanzia Aprili 27 mpaka 29, hivyo ni haki kwa kila mgombea kufanya kile anachokiamini, milango ipo wazi kwa atakayeshinda atarudishwa kwenye mchakato,” alisema Mchungahela.

LUNYAMADZO MLYUKA, Dar es Salaam

Comments are closed.