The House of Favourite Newspapers

Wanafunzi wa ualimu 382 kati ya 7805 ndiyo wenye vigezo kurudi UDOM

0
profjoycendalichakoMay 28 2016 Serikali iliwarejesha nyumbani wanafunzi 7,805 waliokuwa wanasoma Stashahada Maalum ya Ualimu wa Sayansi na Hisabati Chuo Kikuu Dodoma.
Wanafunzi waliosimamishwa masomo walikuwa wamegawanyika katika makundi makuu mawili. Kundi la kwanza lilikuwa ni wanafunzi 6,595 waliodahiliwa katika Stashahada Maalumu ya Ualimu wa Elimu ya Sekondari na kundi la pili lilikuwa na wanafunzi 1,210 waliodahiliwa katika mafunzo ya Stashahada ya Ualimu wa Elimu ya Msingi.
Taarifa iliyotolewa leo na waziri wa Elimu, Sayansi, Teknolojia na Mafunzo ya Ufundi, Joyce Ndalichako amesema kwamba baada ya hatua ya kuwaondoa wanafunzi chuoni kuchukuliwa, Serikali ilifanya  Uchambuzi wa wanafunzi hao kwa lengo la kujiridhisha na sifa zao.  Baada ya uchambuzi huo leo July 19 2016 Serikali imetangaza maamuzi haya…….
Kundi la Stashahada Maalumu ya Ualimu wa Elimu ya Sekondari
Serikali imesema kwa kuwa uchambuzi umebainisha kuwa Wanafunzi wenye ufaulu wa Daraja la I na la II ambao pia wamefaulu masomo mawili ya Sayansi kwa kiwango cha C-A ni 382 (mwaka wa I -134 na mwaka wa II – 248), wanafunzi hao ndiyo pekee watakaorudishwa katika Chuo Kikuu cha Dodoma ili wakamalizie mafunzo yao katika Chuo hicho.
Wanafunzi 4,586 wa mwaka wa I wa Programu Maalum ya Stashahada ya Ualimu wa Elimu ya Sekondari waliokidhi vigezo vya ufaulu watahamishiwa katika Vyuo vya Ualimu vya Morogoro, Butimba, Mpwapwa, Songea na Tukuyu kuendelea na masomo yao.
Wanafunzi 1,337 wa Mwaka II watahamishiwa kwenye Vyuo vya Ualimu vya Korogwe na Kasulu kumalizia masomo yao.
Wanafunzi 290 waliokuwa wamedahiliwa kusoma Programu Maalum ya Stashahada ya Ualimu wa Elimu ya Sekondari Masomo ya Sayansi na Hisabati ambao hawana sifa stahiki wanashauriwa kuomba mafunzo yanayolingana na sifa walizo nazo kwenye chuo chochote wanachotaka wao.
Kundi la Programu ya Ualimu wa Elimu ya Msingi
Serikali imesema wanafunzi katika kundi hili hawakuwa sehemu ya program maalum ya kupunguza uhaba wa walimu wa Sekondari wa Sayansi na Hisabati. Walikuwa wanaandaliwa kufundisha shule za msingi wakati lengo la Programu Maalum ilikuwa ni kukabiliana na tatizo za uhaba wa walimu wa Sekondari. Maudhui ya program waliyokuwa wanasoma hayakuwa sawasawa na yale ya Programu ya Ualimu wa Sekondari wa Sayansi na Hisabati.
Wanafunzi 29 wa mwaka wa II wenye Cheti cha Daraja IIIA waliodahiliwa kusoma Stashahada ya Ualimu wa Shule za Msingi watahamishiwa katika Chuo cha Ualimu Kasulu wamalizie masomo yao kwa gharama zao wenyewe.
Wanafunzi 1,181 waliodahiliwa kusoma Stashahada ya Kawaida ya Ualimu wa Elimu ya Msingi waombe mafunzo yanayolingana na sifa walizonazo mahali popote watakapotaka wao.
Aidha Serikali imesema itaendelea kuwapatia mikopo wanafunzi watakaorejeshwa UDOM na wanafunzi watakaohamishiwa kwenye Vyuo vya Ualimu vya Serikali watapewa mkopo wa kiasi cha Sh. 600,000/= kwa mwaka ambayo ni ada ya Mafunzo ya Ualimu itakayolipwa moja kwa moja Chuoni.
Leave A Reply