Zelensky Ampigia Simu Rais wa Senegal, Ataka Kuongea na Umoja wa Afrika
RAIS wa Ukraine Volodymyr Zelensky amewasiliana na rais wa Senegal Macky Sall ambaye ndiye Mwenyekiti wa Umoja wa Afrika (AU) kuelezea adhima yake ya kutaka kuhutubia Umoja huo na kuelezea athari za vita ya Ukraine na Urusi kwa uchumi wa nchi za Afrika.
Sall amethibitisha kupokea simu kutoka kwa Zelensky ambaye amekuwa akipaza sauti kwa viongozi wa mataifa mbalimbali duniani kuwaelezea namna ambavyo Ukraine inapambana na uvamizi wa Urusi lakini madhara yanayosababishwa na majeshi ya Urusi nchini mwake.
“Tulijadiliana kuhusu madhara ya vita ya Ukraine kwa uchumi wa dunia na kuangalia namna ya kutafuta njia sahihi ya maridhiano ili kumaliza mgogoro huo.” Alisema Sall.
Mazungumzo ya Sall na Zelensky yanaungana na msimamo wa kauli ya Umoja wa Afrika iliyotolewa Februari 24, kutaka kusitishwa kwa mapigano mara moja kati ya Ukraine na Urusi na kurudi katika meza ya mazungumzo ili kumaliza tofauti zao.
Licha ya kwamba mataifa mbalimbali ya Afrika yanaiunga mkono Ukraine hasa kwenye vikao vya Umoja wa Mataifa katika dhana ya kutetea mipaka ya nchi yake lakini bado kumekuwa na hali ya kutofungamana na upande wowote katika dhana nzima ya mgogoro unaoendelea baina ya nchi hizo mbili.
Huku vita hiyo ikiwa ndani ya wiki ya saba hadi sasa kwa mujibu wa takwimu za Umoja wa Mataifa ni kwamba jumla ya watu milioni 4.3 wamekimbia makazi yao nje ya nchi na Zaidi ya wengine milioni 7.1 wametawanyika na kukimbia makazi yao ndani ya nchi ya Ukraine.
Zelensky amesema maelfu ya watu wamefariki japo hakuna idadi kamili ya waliojeruhiwa kutokana na vita hiyo.