The House of Favourite Newspapers

Simba Yabadili Mfumo Kuiua Azam

0
Wachezaji wa Simba wakiendelea kufanya mazoezi.

 

SAA chache kabla ya mchezo wa Ligi Kuu Bara kati ya Azam FC dhidi ya Simba kesho Juma­mosi kwenye Uwanja wa Azam Complex, kuna mambo yameibuka na inavyoonekana ushindani utakuwa mkali kutokana na upepo ulivyo kwa timu zote hizo.

Mchezo huo unatarajiwa kuwa mgumu kwa kuwa kila upande umejipanga vizuri na umekuwa ukijinadi kuwa upo vizuri lakini gumzo zaidi ni kitendo cha mchezo huo kuchezwa kwenye uwanja huo maarufu kwa jina la Uwanja wa Chamazi, ambao unamilikiwa na Azam FC, ikiwa ni mara ya kwanza baada ya kupita kipindi cha muda mrefu tangu Simba walipocheza kwenye dimba hilo mchezo wa ligi kuu.

Akizungumzia mchezo huo, Ofisa Habari wa Simba, Haji Manara, amesema kuwa wanajua uwanja huo sehemu ya kuchezea ‘pitch’ ni ndogo tofauti na ulivyo Uwanja wa Taifa ambao wamekuwa wak­iutumia kama uwanja wao wa nyumbani, lakini kuna mikakati mizuri wameipanga kuhakiki­sha wanapata ushindi.

Mazoezi yakiendlea.

Akifafanua zaidi Manara alisema: “Tunajua uwanja wao ni mdogo tofauti na Taifa lakini kocha wetu Joseph Omog ni kocha mkongwe na wa kimataifa, ameshawahi kui­fundisha Azam kwa mafanikio, anaujua uwanja wao vizuri.

“Hivyo alichoamua kufanya ni kubadili mbinu ili timu iweze kucheza soka lina­loendana na uwanja, unajua Simba tumeshazoea kucheza soka la kutanua uwanja, sasa mbinu za jinsi ya kuutumia Uwanja wa Azam Complex zimeshafanyika na tunaamini tutaibuka na ushindi.

“Tuna mifumo mipya kwa ajili ya uwanja huo, tunaamini tutaibuka na ushindi.”

Katika mazoezi ya jana ya timu hiyo, straika John Bocco wa Simba alifanya mazoezi kama kawaida na kuna uwezekano mkubwa akacheza katika mchezo huo.

Kuhusu mapato

Manara pia alizungumzia suala la mapato kwa kusema kuwa ni vema Shirikisho la Soka la Tanzania (TFF) likaa­mua mfumo wa kuifanya timu ya nyumbani kubeba mapato yote ya mchezo, hoja ambayo ilijibiwa na Ofisa Habari wa TFF, Alfred Lucas aliyesema suala hilo anatakiwa kuliwa­silisha katika mamlaka husika na linaweza kufanyiwa kazi kuanzia msimu ujao kwa kuwa tayari msimu wa sasa umeshaanza.

Okwi, Juuko ndani ya nyumba

Aidha, Manara alisema wachezaji wao wa kimataifa raia wa Uganda, Emmanuel Okwi na Juuko Murshid walitarajiwa kuwasili jana mchana kujiunga na timu hiyo wakitoka kwenye majukumu ya timu ya taifa na hivyo wa­nategemewa kuwepo katika mchezo wa kesho.

Kuhusu beki wao Shomari Kapombe, alisema anaen­delea vizuri wakati kipa wao Said Mohamed ‘Nduda’ anatarajiwa kuondoka wik­iendi hii baada ya safari yake kuchelewa kutokana na suala la visa.

Azam nao watoa neno

Ofisa Habari wa Azam FC, Jaffar Idd upande wake alisema wamefurahishwa na uamuzi wa TFF kupeleka mch­ezo huo uwanjani hapo na kusisitiza maandalizi yapo na wanaamini watautumia vema uwanja wao.

Kuhusu Tshishimbi

Wakati huohuo, Manara amesema kitendo cha baadhi ya mashabiki wa soka kum­shambulia kuhusu ulemavu wake wa ngozi siyo uanamich­ezo na kuwataka wataniane kwa hoja za kishabiki na siyo kuhusu ulemavu wa mtu.

Manara amesema hayo baada ya hivi karibuni kuibuka kwa kashfa nyingi dhidi yake kutokana na yeye kutumia kurasa zake za kijamii kumta­nia kiungo wa Yanga, Papy Tshishimbi ambapo amekuwa akiweka picha zinazoonyesha kuna watu wanamuita mche­zaji huyo Shishi Baby.

“Mimi nimeshazoea utani, kuna vitu ambavyo wao wa­navuka mipaka, utani katika soka ni kitu cha kawaida na hata nilichofanya sikuwa na maana mbaya, lakini wao wanaanza kutukana kuhusu ulemavu, naweza kuvumilia vipi kuhusu hao wengine wenzangu ambao nao wana hali kama mimi.

“Nafikiri kwa kuwa kuna namba zao za simu mitandao­ni hao wanaotukana ni vema jeshi la polisi likafanyia kazi suala hilo.”

Stori: Khadija Mngwai na Ibrahim Mressy | Championi

Leave A Reply