KATIKA kuhakikisha wanafanikiwa kumpata mpachika mabao wa Tanzania Prisons, Mohammed Rashid, Yanga imepanga kumtumia waziri mmoja aliyepo chini ya Rais wa Jamhuri Muungano ya Tanzania, John Magufuli kwa ajili ya kufanikisha saini ya nyota huyo.
Mohammed anachuana vikali na mshambuliaji wa Simba, Mganda, Emmanuel Okwi mwenye mabao 8 katika ufungaji wa Ligi Kuu Bara huku yeye akifuatia akiwa na mabao 6.
Mshambuliaji huyo, anaichezea Prisons inayomilikiwa na Jeshi la Magereza la mkoani Mbeya.
Gazeti hilo limepata taarifa kuwa viongozi wa Yanga wamepanga kumfuata waziri huyo kwa ajili ya kuwarahisishia kumpata Mohammed.
Mtoa taarifa huyo alisema, wamefikia hatua za kumtumia waziri huyo kutokana na mshambuliaji huyo kuwa ameajiriwa na Jeshi la Magereza mkoani Mbeya.
“Kocha ametoa mapendekezo kadhaa ya kuimarisha kikosi chetu na kati ya hizo ni safu ya ushambuliaji, mchezaji ambaye anaweza kuwa chaguo sahihi kwetu ni huyo wa Prisons lakini kumpata ni jambo gumu, tunasubiri kuwasilina na waziri atusaidie,” alisema mtoa taarifa huyo.
Upande wa Yanga kupitia kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili, Hussein Nyika alisema: “Tumepanga kufanya usajili wa kimyakimya.”
Wakati huohuo, uongozi wa Simba nao unadaiwa kujipanga kumsajili mchezaji huyo kutokana na kasi ya mabao kuwa ndogo kikosini kwao.
Mmoja wa viongozi wa Simba aliyeomba hifadhi ya jina lake, amesema wanaamini usajili huo utaongeza nguvu Simba.
Alipoulizwa suala hilo, Kaimu Makamu wa Rais wa Simba, Idd Kajuna, alisema bado hawajaanza usajili, hivyo endapo wataanza kila kitu kitajulikana.
Alipotafutwa Katibu Mkuu wa Prisons, Havinitishi Abdallah alisema: “Sijui kama tunaweza kumwachia mchezaji huyo, kwani tunamtegemea katika kikosi chetu lakini pia bado hajakomaa.
“Kwa umri wake alionao tukimwachia akajiunge na timu hiyo ama Yanga hakika atakuwa anaenda kujichimbia kaburi, hatutaki akapotee.”