WIKIENDI hii inatarajiwa kuwa ya burudani kubwa pale klabu kongwe za Simba na Yanga zitakapokutana kwenye Uwanja wa Taifa jijini Dar es Salaam.
Timu hizo, zinatarajiwa kukutana katika mechi ya Ligi Kuu Bara mchezo unaotarajiwa kujaa upinzani mkubwa.
Katika mechi hiyo, Simba itaingia uwanjani ikiwa inaongoza katika msimamo wa ligi ikiwa na pointi 59 huku Yanga ikifuatia ikiwa na 48.
Pambano hilo linatarajiwa kuwa la kisasi kwa kila moja kutaka ushindi ili itengeneze rekodi kubwa ambayo haitafutika katika historia ya soka.
Mara kadhaa timu hizo zinapokutana huwa yanajitokeza matukio mengi ya ndani na nje ya uwanja ikiwemo watu kuzimia na wengine hata kufariki dunia.
Nije kwenye mada yangu ya leo, hii ni kuwatahadharisha mashabiki wa timu hizo zote mbili za Simba na Yanga kuwa zisifike uwanjani hapo na matokeo yao mfukoni.
Siku zote mchezo wa soka una dakika 90 pekee ambazo ndiyo zinaamua pambano na siyo kitu kingine katika mechi.
Lakini wapo baadhi ya mashabiki wenyewe wanakwenda uwanjani wakiwa na matokeo yao kuwa timu yangu inashinda kitu ambacho siyo sahihi.
Na hicho ndiyo chanzo cha mashabiki hao kuzimia uwanjani, hivyo mashabiki wanachotakiwa ni kuiepuka hali hiyo ya kuiamini timu kwamba itapata matokeo ya ushindi tu na si vingine.
Kwani mara kadhaa timu hizo zikikutana huwa hazitabiriki, hasa kwenye suala la matokeo, hata kama timu moja inakuwa ipo vizuri kwa maana ya usajili mzuri na ipo kwenye kiwango cha hali ya juu.
Shabiki hutakiwi kuipa asilimia 100 timu yako kuwa itapata ushindi na uzuri historia ya timu hizi mbili zinajulikana wazi, hivyo waende uwanjani wakijua mpira ni dakika 90.
Lipo wazi, timu hizo zinapokaribia kukutana zinaongeza muda wa maandalizi mfano mzuri timu hizo zimepitiliza kambini Morogoro zote zikitokea kwenye mechi zao za mwisho za ligi.
Simba na Yanga mara mwisho kukutana ilikuwa katika mzunguko wa kwanza ambapo mchezo ulimalizika kwa sare bao 1-1.
Katika mechi hiyo, tuliona mashabiki wengi wa Simba wakiujaza uwanja kwa matumaini ya kupata ushindi kutokana na uimara wa kikosi chao.
Kama nilivyosema awali, soka ni mchezo wa dakika 90, hali ya mambo ikabadilika kwa Yanga katika mechi hiyo kucheza kwa kiwango cha juu tofauti na wenyewe walivyotarajia, hivyo waliangalie hilo mashabiki wa timu hizo.
Achana na hilo, nirudi kwa waamuzi wa mchezo huo kwa kuwaambia kuchezesha kwa haki bila ya kupendelea timu yoyote ili mshindi apatikane kwa haki.
Kikubwa waamuzi hao wanatakiwa kuchezesha kwa kufuata sheria 17 za mchezo huo ili kufanikisha hilo, kwani ninaamini kila timu imefanya maandalizi ya kutosha ya mchezo huo.
Mechi hiyo huenda ikaharibiwa na waamuzi kama wasipokuwa makini kutokana na upungufu watakaoufanya na kusababisha fujo zisizokuwa na maana uwanjani hapo.
Hivyo basi ni wajibu wa timu zote mbili kuwa makini katika mchezo huo ili mshindi apate matokeo kwa uhalali na kwa upande wa wachezaji, waangalie zaidi mchezo kuliko kukamiana na kuumizana.
Kikubwa wachezaji hao wanatakiwa kufahamu kuwa licha ya upinzani wa Simba na Yanga, watu wanahitaji kuangalia soka la ushindani bila ya kutokea fujo ya aina yoyote itakayoharibu ladha au burudani.
Hali hiyo ya fujo, pia inawahusu mashabiki kwani mara kadhaa kumetokea uvunjwaji wa amani kwa maana ya mashabiki kufanya vitendo vibaya.
Kwani mashabiki hao wamekuwa wakifanya vitendo vya uvunjaji amani kwa kuvunja viti na kuving’oa kwa makusudi pale wanapoona timu yao inapata matokeo mabaya au mwamuzi anapofanya maamuzi ambayo siyo sahihi.
Kama atatokea shabiki ambaye hataweza kujikontroo wakati mechi hiyo inaendelea pale maamuzi yanapotolewa na mwamuzi basi ni vema akaondoka zake uwanjani hapo kwa usalama wake.
Au kama ataona atashindwa kabisa, basi ni bora akabaki nyumbani kufuatilia pambano hilo kupitia televisheni, ninaamini jeshi la polisi litakuwa limejiandaa kulinda usalama uwanjani hapo.
Nimalizie kwa kuwaambia kuwa kila shabiki anatakiwa kuwa mlinzi wa mwenzake kwa kila tukio la uvunjwaji amani akilifanya kwani uwanja ni mali yetu wenyewe.
Nimalizie kwa kumkumbusha mwamuzi atakayechezesha mchezo huo kuwa makini kwa kuhakikisha anajitahidi kuchezesha kwa kufuata sheria 17 za soka ili kuondoa malumbano ya hapa na pale yanayoweza kusababisha fujo uwanjani.
Comments are closed.