The House of Favourite Newspapers

Championi Lambana Hans Poppe, Asisitiza Hajakimbia

Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe.

BAADA ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar kutoa amri ya kukamatwa kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe, mwenyewe ameibuka na kufun­guka hajakimbia kesi kama inavyodaiwa isipokuwa yupo nchini India kwa matibabu ya goti la mguu wake linalomsumbua.

 

Hivi karibuni ma­hakama hiyo nchini ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba, ilitoa amri ya kukamatwa kwa mwenyekiti huyo na Franklin Lauwo na wafikishwe mahakamani hapo kuunganishwa ka­tika kesi ya utakatishaji fedha inayomkabili rais wa timu hiyo, Evans Aveva na makamu wake, Geofrey Nyange ‘Kaburu’.

 

Championi Jumatatu lilifanikiwa kumpata mwenyekiti huyo am­bapo mahojiano mafupi yalikuwa kama ifuat­avyo.

Championi: Habari yako kiongozi?

 

Poppe: Salama, nashukuru Mungu naendelea vizuri.

Championi: Kikubwa ni kutaka kufahamu unazung­umziaje kasi ya Simba katika mechi zilizobaki kuelekea kutwaa ub­ingwa wa msimu huu maana umekuwa kimya sana tofauti na kawaida yako.

 

Poppe: Nipo kimya kwa sababu niko zangu India nimekuja kupata matibabu hivyo siwezi kuon­gelea mambo ya Simba kwa kuwa sijui yana­vyokwenda kwa sasa.

 

Championi: Matibabu ya kitu gani?

Poppe: Goti la mguu wangu linanisumbua licha ya ku­fanyia upa­suaji Novemba, mwaka jana, sasa nimeona bora nije huku India wanishu­ghulikie tena na bado naendelea na matibabu, bado sijamaliza.

 

Championi: Lakini Ma­hakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imetoa amri ukamat­we ili uunganishwe kwenye kesi ya rais wa Simba na makamu wake, unazung­umziaje hilo.

 

Poppe: Bado sijapata taarifa rasmi zaidi ya kusoma kwenye mi­tandao kama natakiwa kukamatwa kwa amri ya mahakama, lakini ifahamike kuwa sijakimbia nipo huku kwa ajili ya kupata matibabu ya goti langu, nikimaliza nitarudi zangu nyumbani kwa sababu hata visa yangu ya kujia huku nime­chukulia hapo Dar kwa sababu vielelezo vyote ninavyo, sasa kwa nini nikimbie?

 

Championi: Asante kwa ushirikiano na pole kwa kuumwa.

Hans Poppe: Asante

 

Ikumbukwe awali kab­la ya kuongezwa Poppe na mwenzake, Aveva na Kaburu walikuwa wa­nakabiliwa na mashtaka matano ya kughushi, kuwasilisha nyaraka za uongo na kutakatisha fedha kiasi cha dola 300,000 (Sh 683,115,000) za Kimarekani kabla ya kuongezewa mengine matano na kufikia kumi.

Stori: Ibrahim Mussa ,Dar es Salaam

Comments are closed.