BAADA ya Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu jijini Dar kutoa amri ya kukamatwa kwa Mwenyekiti wa Kamati ya Usajili ya Simba, Zacharia Hans Poppe, mwenyewe ameibuka na kufunguka hajakimbia kesi kama inavyodaiwa isipokuwa yupo nchini India kwa matibabu ya goti la mguu wake linalomsumbua.
Hivi karibuni mahakama hiyo nchini ya Hakimu Mkazi Mkuu, Thomas Simba, ilitoa amri ya kukamatwa kwa mwenyekiti huyo na Franklin Lauwo na wafikishwe mahakamani hapo kuunganishwa katika kesi ya utakatishaji fedha inayomkabili rais wa timu hiyo, Evans Aveva na makamu wake, Geofrey Nyange ‘Kaburu’.
Championi Jumatatu lilifanikiwa kumpata mwenyekiti huyo ambapo mahojiano mafupi yalikuwa kama ifuatavyo.
Championi: Habari yako kiongozi?
Poppe: Salama, nashukuru Mungu naendelea vizuri.
Championi: Kikubwa ni kutaka kufahamu unazungumziaje kasi ya Simba katika mechi zilizobaki kuelekea kutwaa ubingwa wa msimu huu maana umekuwa kimya sana tofauti na kawaida yako.
Poppe: Nipo kimya kwa sababu niko zangu India nimekuja kupata matibabu hivyo siwezi kuongelea mambo ya Simba kwa kuwa sijui yanavyokwenda kwa sasa.
Championi: Matibabu ya kitu gani?
Poppe: Goti la mguu wangu linanisumbua licha ya kufanyia upasuaji Novemba, mwaka jana, sasa nimeona bora nije huku India wanishughulikie tena na bado naendelea na matibabu, bado sijamaliza.
Championi: Lakini Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu imetoa amri ukamatwe ili uunganishwe kwenye kesi ya rais wa Simba na makamu wake, unazungumziaje hilo.
Poppe: Bado sijapata taarifa rasmi zaidi ya kusoma kwenye mitandao kama natakiwa kukamatwa kwa amri ya mahakama, lakini ifahamike kuwa sijakimbia nipo huku kwa ajili ya kupata matibabu ya goti langu, nikimaliza nitarudi zangu nyumbani kwa sababu hata visa yangu ya kujia huku nimechukulia hapo Dar kwa sababu vielelezo vyote ninavyo, sasa kwa nini nikimbie?
Championi: Asante kwa ushirikiano na pole kwa kuumwa.
Hans Poppe: Asante
Ikumbukwe awali kabla ya kuongezwa Poppe na mwenzake, Aveva na Kaburu walikuwa wanakabiliwa na mashtaka matano ya kughushi, kuwasilisha nyaraka za uongo na kutakatisha fedha kiasi cha dola 300,000 (Sh 683,115,000) za Kimarekani kabla ya kuongezewa mengine matano na kufikia kumi.
Stori: Ibrahim Mussa ,Dar es Salaam
Comments are closed.