The House of Favourite Newspapers

Yanga Yaweka Rekodi Mbaya Afrika

WAWAKILISHI wa Tanzania katika Kombe la Shirikisho Afrika, Yanga, wameanza vibaya michuano hiyo kufuatia kuweka rekodi mbaya katika mechi za kwanza za hatua ya makundi ya michuano hiyo zilizochezwa wikiendi iliyopita.

 

Katika mechi zote zilizochezwa wikiendi iliyopita za michuano hiyo, Yanga ndiyo timu pekee iliyofungwa idadi kubwa ya mabao baada ya kukubali kichapo cha mabao 4-0 kutoka kwa USM Alger ya Algeria.

 

Yanga katika hatua hiyo ya makundi imepangwa Kundi D, sambamba na Rayon Sport ya Rwanda, Gor Mahia kutoka Kenya na USM Alger.

 

Katika mechi hiyo iliyopigwa kwenye Uwanja wa Stade 5 Juillet 1962 nchini Algeria, Yanga ndiyo ilikubali kichapo hicho, huku Rayon Sport ikiwa katika uwanja wake wa nyumbani wa Nyamirambo, Kigali, Rwanda, ikilazimishwa sare ya bao 1-1 dhidi ya Gor Mahia ya Kenya.

 

Kutoka Kundi A, Asec Mimosas ya Ivory Coast ilifanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 1 – 0 dhidi ya Aduana Stars kutoka Ghana wakati Raja Casablanca ikitoka sare ya bila kufungana na AS Vita katika mchezo uliopigwa Morocco huku katika mechi za Kundi B, Renaissance Sportive de Berkane ilifanikiwa kushinda bao 1-0 dhidi ya El Hilal kutoka Sudani kwenye mchezo uliopigwa nchini Burkina Faso na Al Masry ikishinda mabao 2-0 dhidi ya União Desportiva do Songo katika mchezo uliopigwa nchini Misri.

 

Mechi za Kundi C kwenye michuano hiyo, Enyimba FC ilifanikiwa kuibuka na ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Djoliba AC de Bamako katika mchezo uliopigwa nchini Nigeria wakati Williamsville katika kundi hilo ilifanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Cara Brazzaville kwenye mchezo uliopigwa nchini Ivory Coast.


 

Comments are closed.