Bocco Aichimba Mkwara Ndanda
JOHN Bocco ambaye ni nahodha wa Simba, amesema kocha wao, Mbelgiji Patrick Aussems amewapa mbinu mpya za kuhakikisha wanapa ushindi kwenye mechi za ugenini kuanzia ya leo dhidi ya Ndanda FC.
Simba ambayo mpaka sasa imecheza mechi mbili na kushinda zote, inatarajiwa kucheza mchezo wake wa kwanza ugenini kwenye Uwanja wa Nangwanda Sijaona mkoani Mtwara dhidi ya Ndanda.
Bocco ambaye ni mmoja kati ya washambuliaji warefu Bongo, ameliambia Championi Jumamosi kuwa, kikosi chao kipo katika hali nzuri na wachezaji wote wana morali ya kuhakikisha wanaondoka na pointi tatu huku kocha akiwaongezea mbinu za namna ya kupata matokeo wakiwa ugenini
“Tunawaheshim sana wapinzani wetu Ndanda na hilo lipo wazi ni lazima umuheshimu mpinzani wako unayecheza naye kwani naye amefanya maandalizi ya kutosha kujiandaa na mchezo huo.
“Pia, sisi chini ya kocha wetu Aussems (Patrick) tumejiandaa vya kutosha kwa kutupa mbinu mbalimbali za kucheza mechi za ugenini ili tupate matokeo, hivyo hatuna hofu ya mchezo huo.
“Kikubwa tunawaomba mashabiki wa Simba kujitokeza kwa wingi kwa ajili ya kuisapoti timu yao itakapokuwepo uwanjani ikipambana kwani bila ya wao sisi hatuwezi kufanya vizuri,” alisema Bocco.
Comments are closed.