The House of Favourite Newspapers

JERRY MURO ATAFUNA MFUPA WA MGOGORO WA ARDHI SELASI SING’ISI

Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Mhe Jerry Cornel Muro akizungumza jambo.
Baadhi ya wanananchi wakisikiliza mkutano huo.
Mmoja wa wanannchi akiuliza swali.

Mkuu wa Wilaya ya Arumeru, Jerry Cornel Muro, anakusudia kupeleka ombi kwa Rais wa Jamhuri ya muungano Mhe ,Dkt. John Pombe Magufuli la kufuta hati za baadhi ya mashamba makubwa ardhi ambayo wamiliki wake wamebainika kuwa chanzo cha kuvuruga amani na usalama kutokana na kuwepo kwa migogoro ya muda mrefu ambayo baadhi imegharimu maisha ya wananchi pamoja na uharibifu wa mali.

 

 

Mhe muro ametoa kauli hiyo wakati alipofanya ziara ya utatuzi wa mgogoro wa ardhi katika kata ya Selasi Sing’isi ambayo ina migogoro mikubwa ya ardhi baina ya wananchi waliovamia mashamba ya Wizara ya Kilimo pamoja na mashamba ya wawekezaji ambayo yamesababisha madhara makubwa ya kuuwawa kwa wananchi wawili huku mali zikiharibiwa vibaya pamoja kukosekana kwa amani kwa muda wa zaidi ya miaka 5 .

 

 

Mhe Muro ambaye alilazimika kutembea kwa miguu katika kata nzima ameshangazwa kuona wananchi wengi wenye uwezo wa kulima wakishindwa kulima kutokana na baadhi ya wawekezaji na wamiliki wa maeneo hayo kushindwa kuyaendeleza hatua iliyosababisha wananchi kuamua kuvamia mashamba hayo na kulima kienyeji hatua ambayo imeibua migogoro mikubwa ya ardhi, ambapo amesisitiza dhamira ya Serikali ni kuhakikisha wawekezaji wanawekeza kwa nia ya dhati na sio kuhodhi mashamba makubwa ambayo wameshindwa kuyaendeleza na hatimaye kutoa mwanyakKwa wananchi kuvamia na kisha kuibua migogoro.

 

 

Akizungumza katika mkutano wa hadhara baada ya kukagua maeneo hayo katika viwanja vya chama cha Ushirika Sing’isi Mhe Muro amesema katika hatua za awali ametumia busara ya kumtaka ndugu Aloyce Kimaro mmiliki wa Hotel ya Nakara kutokanyaga eneo la Madira Sing’isi alilokuwa akitaka kubadilisha matumizi ya Ardhi hatua iliyosababisha kuibuka kwa vurugu kubwa zilizosababisha vifo pamoja na uharibifu wa mali katika eneo hilo ambalo hapo awali ndugu Kimaro alipewa eneo hilo na Wizara ya Kilimo kwa ajili ya uwekezaji wa hotel kubwa na amesema taarifa zinaonyesha kuwepo na viashiria vya uvunjifu wa Amani endapo ndugu Kimaro atarejea katika eneo hilo kwani taarifa za awali zinaonyesha kuwepo kwa utata wa njia alizotumia kumilikishwa shamba hilo na kuviagiza vyombo vya ulinzi na usalama kuendelea kulichunguza jambo hilo kwa umakini mkubwa.

 

 

Mhe Muro ambaye aliongozana na viongozi wa kamati ya wananchi waliounda wakati wa ziara ya mkuu wa mkoa wa Arusha ya kushughulikia migogoro ya ardhi katika kata hiyo, Dc Muro ameagiza wananchi kupewa hekari 66 kati ya hekari 92 walizokuwa wanapaswa kupewa na Halmashauri ikiwa ni sehemu ya Ardhi iliyotolewa na wizara ya Kilimo na kuagiza mchakato wa kutafuta hekari zingine 25 zilizobaki uendelee kwa haraka ili wananchi wapate maeneo ya kulima hatua itakayoondoa migogoro ya wananchi kuvuamia maeneo mengine ya Wizara ya Kilimo ambayo yanetengwa kwa shughuli za kilimo.

 

 

Muro pia amekiri kuwepo kwa utata wa umiliki wa eneo hilo kama ambavyo imejionyesha katika ziara yake na kuviagiza vyombo vya usalama ikiwemo takukuru kuaendelea na uchunguzi ambao ulishaanza lakini safari hii ametaka uchunguzi uwe wa kasi kidogo kutokana na kuwepo kwa taarifa za awali zinaonyesha kufanyika kwa miamala ya fedha kutoka kwa  Kimaro kwenda kwa baadhi ya wananchi ambao wanatajwa kuwa vinara wa kuchochea mgogoro huo wa ardhi ili kuondoa amani katika kata ya Selasi Sing’isi ambapo Muro alivitaka vyombo vya usalama pia kuwachukua watuhumiwa hao wawili kwa hatua za uchunguzi zaidi.

 

Akizungumza katika Mkutano wa Hadhara Diwani wa kata ya Sing’isi pamoja na viongozi wa kamati ya wananchi iliyoundwa kumaliza mgogoro huo ambao pia ulihusisha viongozi kutoka makao makuu ya Wizara ya Kilimo wote kwa pamoja mbali na kupongeza juhudi zilizofanywa na mkuu wa mkoa wa Arusha Mhe Mrisho Gambo pamoja na Mkuu wa Wilaya ya Arumeru Mhe Jerry Muro za kumaliza mgogoro huo walikubaliana kutoa Azimio la kumaliza mgogoro huo baada ya mazungumzo ya Hekima na busara ya pande zote zinazovutana katika mgogoro huo.

 

Mgogoro huo ambao umedumu kwa zaidi ya miaka 10 umesababisha hasara kubwa ya vifo vya wananchi wasiokuwa na hatia, uharibifu wa mali pamoja na maeneo hayo kutokutimika ipasavyo ambapo kwa Wizara ya Kilimo peke yake umeleta hasara ya zaidi ya Bilioni 8 , huku wananchi na mwekezaji wakipata hasara ambayo hata hivyo tathmini ya awali inaonyesha ni zaidi ya Bilioni 3 na kusababisha jumla ya hasara kuwa zaidi ya Bilioni 11.

 

Mkuu wa Wilaya ya Arumeru amemaliza ziara yake ya kata ya Selasi Sing’isi pia kwa kutoa maelekezo ya baadhi ya wananchi zaidi ya elfu moja ambao walikuwa wameuziwa viwanja na kupewa hati za makazi katika maeneo ya chini kujitokeza na kuanza kuendeleza maeneo yao kwa kuwa mgogoro umemalizika na amani imerejea tena.

 

 

Imetolewa na ofisi ya Mkuu wa Wilaya ya Arumeru , ARUSHA
24/10/2918

 

Comments are closed.