The House of Favourite Newspapers

Mahakama Yamrudisha Wambura TFF

Makamu wa Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Michael Wambura.

HATIMAYE Mahakama Kuu ya Dar es Salaam imemrejesha madarakani aliyekuwa makamu wa Rais wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF), Michael Wambura baada ya kutengua maamuzi ya Kamati ya Maadili ya TFF baada ya kumfungia maisha kujihusisha na masuala ya soka.

 

Uamuzi huo umetolewa jana Ijumaa katika Mahakama Kuu na Jaji Benhaji Masoud kufuatia Wambura kuomba mahakama ipitie upya maamuzi ambayo yalitolewa na Kamati ya Maadili ya TFF.

 

Kutokana na maamuzi hayo ya mahakama, Wambura amerejeshwa katika cheo chake cha umakamu wa rais wa TFF na uenyekiti wa Chama cha Soka Mara (FAM).

 

Hata hivyo, wakili wa Wambura, Emmanuel Muga alisema kuwa, kisheria mteja wake hakufungua kesi bali aliomba mahakama ifanye mapitio kutokana na maamuzi ambayo yalikuwa yametolewa na Kamati ya Maadili ya TFF.

 

“Wambura kwa sasa amerejea rasmi TFF na hii ni baada ya Mahakama Kuu ya Dar es Salaam kupitia hukumu ambayo aliomba mahakama iweze kupitia na mteja wangu hakufunguwa kesi sababu anatambua sheria za soka hivyo anarejea katika madaraka yake,” alisema Muga.

 

Kwa upande wa Michael Wambura alisema: “Mahakama imefanya maamuzi sahihi kabisa baada ya kupitia maamuzi nitarudi TFF sababu nilichaguliwa na mkutano mkuu.”

 

Sekretarieti ya TFF ilimfikisha Wambura kwenye Kamati ya Maadili akikabiliwa na tuhuma tatu ikiwemo kupokea fedha za malipo TFF za malipo ambayo hayakuwa halali.

Stori: Martha Mboma, Championi Ijumaa

Comments are closed.