The House of Favourite Newspapers

Zahera: Tutawapiga Lipuli Kiroho Mbaya

KOCHA Mkuu wa Yanga, Mwinyi Zahera, amefunguka kwamba hajali sana timu yake isipopocheza mpira wa kuvutia kwenye Kombe la Shirikisho (FA) kutokana na mechi za kombe hilo kuhitaji zaidi matokeo na siyo kucheza soka.

 

Zahera juzi Jumamosi aliifanikisha Yanga kutinga hatua ya nusu fainali ya kombe hilo baada ya kuwachapa Alliance Schools ya Mwanza kwa penalti 4-3. Bingwa wa kombe hili la Shirikisho atapata nafasi ya kuiwakilisha nchi katika Kombe la Shirikisho Afrika.

 

Akizungumza na Championi Jumatatu, Zahera alisema kwamba michezo ya kombe hilo inahitajika kucheza kwa roho mbaya kutokana na kuhitaji zaidi matokeo ili kusonga mbele, tofauti na kucheza soka la kuvutia, staili ambayo ataitumia katika mechi yake na Lipuli.

 

“Niliwaambia wachezaji tunacheza mechi ya ugenini katika hatua ambayo tunahitaji zaidi matokeo na siyo jambo lingine, hivyo tucheze kwa roho ya kupambana zaidi na hakuna soka la kupendeza.

 

“Mechi za kombe hili kwangu naona hakuna cha kupoteza kwa sababu ukifungwa unatoka na mwenzako anaenda mbele, tunatakiwa kupambana zaidi hasa baada ya kupita hatua hii, lengo ni kuingia fainali na kutwaa taji kwa sababu hii ndiyo njia nyepesi kwetu zaidi ya kucheza michuano ya kimataifa,” alisema Zahera.

 

Yanga kwa sasa watacheza na Lipuli FC katika mechi ya nusu fainali ya kombe hilo katika mechi itakayopigwa Uwanja wa Samora, Iringa.

Comments are closed.